MWENYEKITI wa Chama Cha Wananchi (CUF), ameitaka Serikali kupeleka muswada wa mabadiliko madogo ya katiba ili kupata tume huru ya uchaguzi kabla ya chaguzi zijazo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Prof. Lipumba ametoa kauli hiyo leo tarehe 31 Disemba 2023, akitoa salamu za CUF za kukaribisha mwaka mpya wa 2024.
Prof. Lipumba amesema “Hakuna muswada wa mabadiliko madogo ya Katiba yaliyopendekezaa toka 2014 ili kuingiza uwepo wa tume huru ya uchaguzi na mgombea huru na uchaguzi wa Rais kuhojiwa mahakamani.”
“Natoa wito kwa serikali ya Rais Samia kupeleka muswada wa mabadiliko madogo ya katiba na kurekebisha muswada wa Tume ya Uchaguzi iwe Tume Huru kama ilivyopendekezwa na Mkutano wa Wadau wa tarehe 22-23 Agosti 2023. Ninawatakia Watanzania wote kheri ya mwaka mpya 2024,” amesema Prof. Lipumba.
Mwanasiasa huyo mkongwe nchini Tanzania, amesema ni vyema Serikali ikapeleka muswada wa marekebisho madogo ya Katiba, akidai miswada ya kurekebisha sheria za uchaguzi iliyowasilishwa bungeni jijini Dodoma, Novemba 2023 mapendekezo yake hayatatatua matatizo yaliyojitokeza kwenye chaguzi zilizopita.
Aidha, Prof. Lipumba ameishauri Serikali kuelekea 2024 iweke mikakati ya kutatua changamoto zilizowakabili wananchi 2023, ikiwemo mgawo wa umeme na kupanda gharama za maisha.
Leave a comment