MWENYEKITI wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, amewataka watanzania kutumia nyumba za ibada kuwaombea viongozi wa kisiasa wenye roho ngumu ili Mungu azilegeze ili kupata Tanzania iliyobora. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam …(endelea).
Mbowe ametoa wito huo leo tarehe 31 Disemba 2023 katika harambee ya kukamilisha ujenzi wa awamu ya kwanza ya Kanisa la Bethel lililopo Usharika wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), wa Nshara, Machame mkoani Kilimanjaro.
“Lazima tuombeane, tusaidiane na kupitia kazi ya Mungu tunaweza kufanya mambo makubwa ambayo tunaweza kuona ni magumu katika dunia ya kawaida ya mambo ya kisiasa na kiongozi kwamba kupitia nyumba za ibada tuombe alegeze roho za wale ambao zimekaza ili zilegee ili tukaitafute Tanzania iliyobora zaidi,” amesema Mbowe.
Kuhusu harambee hiyo, Mbowe amesema amefanikiwa kuwafikia marafiki zake 250 akiwemo Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, wabunge na watu kutoka makundi mbalimbali kwa ajili ya kupata michango ya hali na mali kukamilisha ujenzi wa Kanisa hilo.
Mbowe amesema watu wote wameahidi kutoa michango hiyo ambapo kiasi cha fedha kinachohitajika ni Sh. 1.5 bilioni.
Amesema ujenzi huo ukikamilika, katika kanisa hilo kutajengwa chuo cha ufundi kwa ajili ya kutoa ujuzi wa vijana wa usharikani hapo na kutoka maeneo mengine.
Leave a comment