MKUU wa mkoa wa Mwanza, Adam Malima, amesema Serikali imeingia kwenye makubaliano na kampuni ya OA Coal ambayo itajenga mgodi wa pili kwa ukubwa baada ya Geita ambao utakuwa wilaya ya Sengerema. Anaripoti Apaikunda Mosha, TUDARCo … (endelea).
Hayo ameyasema leo Jumatatu ya tarehe 26 Septemba 2022 katika mkutano wa kujadili na kuzitambua fursa zilizopo Mkoa wa Mwanza.
Akizungumza fursa zilizopo katika mkoa huo Malima amesema, wananchi wanatakiwa watambue fursa zilizopo, kuzipokea na kuzichangamkia ili kusaidia ukuaji wa mapato ya uchumi kwa mkoa wa Mwanza na kuwafaidisha wananchi wengine wote.
Akizungumzia sekta ya uvuvi Malima amesema wananchi wametumia vibaya Ziwa Victoria kwani miaka 50 iliopita Ziwa hilo lilikuwa na aina takribani 40 ya Samaki lakini kwa sasa zimebaki aina 5 mpaka 6 ya samaki kutokana na uvuvi haramu.
Pia amesema serikali ya mkoa wa Mwanza imejipanga kuongeza tija katika ufugaji ili waweze kukuza uzalishaji wa maziwa ambayo ni changamoto kubwa kwa wafugaji wengi.
Aidha, amesema pamoja na kuonesha fursa hizo kwa wakazi wa Mwanza jukumu lililopo ni kuwatoa wananchi gizani kwa kufanya utafiti wa masoko na kuwahakikishia uwepo wa masoko ili waongeze jitihada katika utendaji wao.
Leave a comment