MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe amesema 2023 utakuwa mwaka wa kazi ndani ya chama chake, huku akitangaza kufanya operesheni maalum kuanzia ngazi ya jimbo hadi taifa, kwa ajili ya kukiimarisha kuelekea chaguzi zijazo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Mbowe ametoa kauli hiyo jana jioni, akizungumza katika mkutano wa Bunge la Wananchi la Chadema, uliofanyika jijini Dar es Salaam.
“Tunataka tufanye kazi physical, mimi binafisi najitolea 2023 tutafanya operesheni ya jimbo kwa jimbo, kata kwa kata hadi taifa. Naweza kutoa upendeleo hapa kwa wabunge wetu kusema kanda ipi iko tayari kuanza nayo, tuhakikishe kwamba wanachama wanasajiliwa sababu ndugu zangu sio tu tunakwenda kuhuisha chama lakini tunakwenda kusimamia mafunzo na kusimamia uchaguzi,” alisema Mbowe.
Mbowe aliwataka wanachama wa Chadema kushirikiana kwa pamoja kukijenga chama hicho kuelekea Uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa 2024 na Uchaguzi Mkuu wa 2025, hususan katika kutekeleza operesheni yao ya Chadema Digital, akisema itasaidia kukiweza chama hicho kupata ushindi kwenye chaguzi hizo.
Mwenyekiti huyo wa Chadema alisema, licha ya chaguzi zilizopita kuwa misukosuko lakini chama chake kilifanya vizuri kutokana na utekelezaji wa operesheni ya Chadema ni msingi.
“Leo tunapozungumza na wenzetu wanatambua sisi tupo kwenye mitaa hadi Tanzania nzima, ndiyo nguvu ya Chadema na kila chama kingetamani kiwe na nguvu hiyo. Pamoja na nguvu hizo bado hazijatosha kwa hiyo tunakwenda kuanza 2023, matunda ya 2025 yatapatikana kwa kazi kubwa itakayofanyika 2023,” alisema Mbowe.
Mbowe alisema “kwa hiyo kila mmoja wetu kama ana nia ya kuwa mbunge, ajue ni aidha sasa au isiwe. Kila mtu atambue hakutakuw ana njia fupi ya kuwa wabunge, madiwani au mameya kama hatujajipanga 2023. Mwaka wa 2023 unakwenda kuwa mwaka wa kazi.”
Mwanasiasa huyo amewaeleza wanachama wa Chadema kuwa, harakati za mitandaoni hazitasaidia chama chao kushinda chaguzi, bali wanapswa kufika chini kwa wananchi.
“Bila kutambua na kuthamini tunafanya nini makao makuu, kama ninyi huko chini hamkufanya majukumu yenu na kama sisi huku hatutasaidiana na ninyi kusukuma ule wajibu kule chini, hakika tutafika uchaguzi mwingine tutalia tumeibiwa. Zamu hii wao walie kwamba tumenyimwa kura,” alisema Mbowe na kuongeza:
“Hakuna siri ya kujenga siasa bila kuwafikia wapiga kura, hatuwezi kukesha kwenye mitandao ya kijamii tukafikiri ndiyo kampeni za uchaguzi tutadanganyana. Lazima tufike chini tukatambuane mmoja baada ya mmoja.”
Asante ndugu mbowe jaribu kufikiria lenye maana ambalo litaleta faida ktk maisha na wananchi