CHAMA cha ACT Wazalendo kimehitimisha kampeni ya mgombea wake jimbo la Amani leo kwa kuonya kuwa kitazuia hujuma yoyote ya kuvuruga uchaguzi mdogo uliopangwa kufanyika tarehe 17 Diaemba mwaka huu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea).
Kwa mujibu wa hotuba zilizotolewa kwenye mkutano wa hadhara wa kufunga kampeni ulofanyika Uwanja wa Mbarawa, chama hicho hakitaachia hujuma zilizopangwa kwa nia ya kukibeba Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Msimamo huo umekaziwa na Mwenyekiti wa Taifa wa ACT Wazalendo, Juma Haji Duni aliposema uchaguzi huo ni kipimo kizuri kwa Serikali na Tume ya Taifa ya Uchaguzi kama wana nia kweli ya kuendesha uchaguzi wa hishma utakaokidhi vigezo vya kuwa ni uvlchaguzi huru, wa haki na wa kutoa matokeo ya kuaminika.
Duni amesema ipo nafasi ya serikali na taasisi zake kuthibitisha ahadi za kuwepo muelekeo wa siasa za maridhiano kama inavyosemwa na viongozi wakuu wa CCM wakiwemo marais.
Marais Samia Suluhu Hassan wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Hussein Ali Mwinyi wamekuwa wakizungumzia dhamira ya kujenga mazingira ya nchi kuendesha siasa za maridhiano baada ya kupokea ripoti za vikosikazi walivuounda kwa ajili ya kupata maoni ya kufanya mabadiliko ya kisheria na kikatiba nchini.
“Wakati tunasubiri matokeo ya mapendekezo ya wananchi na vyama kuhusu mahitaji ya maridhiano tunaona namna Tume za Uchaguzi zinavyoendesha mambo kinyume cha sheria na katiba. Tunajua mipango ya kuhujumu uchaguzi lakini hatutakubali mipango yao ifanikiwe,” alisema Duni maarufu kama Babu Duni.
Maelezo yake kwenye mkutano wa kampeni yamekuja chama hicho kikiwa kimetoa tamko mapema leo la mwenendo wa Tume kukiuka sheria na katiba ikiwemo Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kukabidhi mamlaka yote ya usimamizi wa uchaguzi huo kwa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC).
Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, Tume ya Taifa ua Uchaguzi ndiyo yenye jukumu la kusimamia uchaguzi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano, Wabunge na Madiwani wa Tanzania.
Mhene Said Rashid, Naibu Katibu wa Mipango na Uchaguzi wa ACT Wazalendo, alitoa tamko mbele ya waandishi wa habari akisema Tume wametangaza daftari la wapigakura ambalo lina baadhi ya watu waliokwishafariki dunia.
“Wakati wa kampeni tumegundua na wananchi wenyewe wametwambia baadhi ya majina yaliyomo kwenye daftari lililotangazwa na Tume wameshaaga dunia.
“Pia kwenye orodha iliyobandikwa tumekuta majina ya watu ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakidai shahada zao za kupigia kura lakini hawajapewa,” alisema.
Wananchi wa jimbo la Amani, ndani ya Wilaya ya Mjini, wanapigakura Jumamosi kumchagua mbunge mpya baada ya aliyetangazwa katika uchaguzi mkuu wa 2020, Maalim Mussa kufariki dunia Septemba mwaka huu.
ACT imemsimamisha mwanachama Mohamed Khamis (Shau) kugombea kiti hicho dhidi ya wagombea 13 akiwemo wa CCM.
Kwa nini tunashindwa kufata katiba ya nchi? Wapi pagumu?
Asante act ktk mashindano kuna mshindi na mshindwa tulikbari ilo na tulielewe ukishinda furahia na ukishindwa kaa kimya