RAIS wa Kenya Uhuru Kenyatta amesema kwamba alikuwa tayari kuachia madaraka baada ya mahakama kuu kufutilia mbali ushindi wake katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2017, ili kuzuia umwagikaji wa damu lakini naibu wake alimshawishi kutofanya hivyo. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Hii ni mara ya kwanza kwa Rais Uhuru kuzungumza yaliyokuwa yakiendelea katika fikra zake baada ya mahakama kuu kufuta ushindi wake na kuagiza marudio ya uchaguzi huo kufuatia kesi ya kupinga matokeo ya kura, iliyowasilishwa katika mahakama hiyo na Raila Odinga na muungano wake wa kisiasa wa NASA.
Uhuru ametoa kauli hiyo jana tarehe 8 Julai, 2022 katika mkutano na viongozi wa kidini kutoka jamii ya wakikuyu, uliofanyika katika ikulu ya rais, jijini Nairobi.
“Nilikuwa tayari kuachia madaraka, kuweka maslahi ya nchi mbele na kuokoa nchi dhidi ya umwagikaji wa damu. Haya madaraka tuliyo nayo hayana thamani sana kushinda maisha ya watu. Ndio! Nilikuwa nimeamua kuachia madaraka na kuokoa nchi,” amesema Uhuru.
Aidha, akizungumzia ujumbe wa sauti ambao umekuwa ukisambaa kwenye mitandao ya kijamii ambapo naibu rais Dk. William Ruto anasikika akisema kwa kejeli kwamba alikuwa alitaka kumzaba kofi Rais Uhuru baada ya mahakama kuu kufutilia mbali ushindi wao.
Uhuru amesema “Iwapo wangenipiga kofi kwa sababu ya madaraka, ningewapa shavu la pili na wapige kofi lingine. Ndio, nilitaka kuachia madaraka na niende Ichaweri (kijijini kwake) kwa sababu nisingeweza kulinganisha madaraka na umwagikagi wa damu.”
Hata hivyo, Ruto ametetea ujumbe huo wa sauti akisema kwamba asingeruhusu Rais Kenyatta kuacha madaraka kwa upinzani ulioongozwa na Raila Odinga.
Leave a comment