KATIKA kampeni ya kuunga mkono jitihada za serikali kwenye matumizi nishati salama kimazingira, kampuni ya sola ya d.light Tanzania Limited imezindua kampeni mpya ya ‘Mwanga Wako, Mchongo Wako’ yenye lengo la kuhamasisha matumizi ya nishati safi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha … (endelea).
Kampeni hiyo ya ‘Mwanga Wako, Mchongo Wako’ itawapatia fursa wateja wenye bahati kujishindia zawadi mbalimbali kama vile mfumo wa nishati ya jua kwa matumizi ya nyumbani watakapolipa siku 90 kwa mkupuo; baiskeli watakapolipa kila siku; simu janja za Infinix Smart 6 4G watakapolipa siku 60 kwa mkupuo; Nokia C2 watakapolipa siku 30 kwa mkupuo, na vifurushi vya muda wa maongezi vya shilingi 20,000 wakimaliza malimbikizo ya mikopo yao.
Thamani ya zawadi zitakazotolewa katika kampeni hii zitakuwa na jumla ya thamani ya Sh. 11 milioni na kampeni hio inatarajiwa kuanza tarehe 14 Agosti, 2023 kwa muda wa miezi miwili, itajumuisha mikoa ambayo ina matumizi makubwa ya nishati ya jua ikiwemo Arusha, Dar es salaam, Geita, Iringa, Katavi, Kilimanjaro, na Lindi.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo jijini Arusha, Mkurugenzi Mtendaji wa d.light Tanzania Limited, Charles Natai amesema kuwa lengo kubwa la kampeni hii ni kuhamasisha watanzania kutumia nishati safi ya sola ili kuleta mapinduzi ya matumizi ya nishati ya jua nchini badala ya nishati zinazohatarisha mazingira na tabaka la Ozoni.
“Kampeni hii inalenga kuwapa hamasa wateja kuhamia kwenye nishati safi na sisi kama d.light tumeona ni vyema kutambua mchango wa kila mteja wa kweli. Hivyo basi, tunapenda kuwataarifu kuwa tutakuwa tunawazadia kila mwisho wa mwezi, hii ni kwa wateja wetu wa sasa ambao bado hawajarudisha mikopo yao au kulipa kwa wakati, lakini pia kwa wateja wapya watakaojiunga nasi. Kama hiyo haitoshi, kutakuwa na zawadi kubwa mwishoni mwa kampeni hii ambapo tutawatangazia Watanzania,” aliongezea Natai.
Kwa upande wake, Madinda Juma ambae ni miongoni mwa wakala wa d.light alisema; “Tangu nimeanza kununua bidhaa za d.light mwaka 2020, imenisaidia kukua kimaisha, nimetoka kipato cha chini hadi leo niko kipato cha kati. Pamoja na yote, nimeweza kujenga nyumba yangu.”
Kampuni hio tayari imewasadia watu zaidi ya milioni 100 barani Afrika na watu wapatao laki mbili nchini Tanzania katika matumizi ya nishati safi ya sola.
Leave a comment