MKUU wa Wilaya ya Momba mkoani Songwe, Faki Lulandala amejitosa katika sakata la mjadala kuhusu mkataba wa uwekezaji kwenye bandari ya Dar es Salaam na kuwataka Watanzania kupuuza upotoshaji unaotolewa na baadhi ya watu wasiokuwa na uzalendo. Anaripoti Ibrahim Yassin…(endelea).
Amesisitiza kuwa uwekezaji katika bandari hiyo ya Dar es Salaam utaziongezea faida wilaya za mkoa wa Songwe hususani Mji wa Tunduma ambao ndio lango la nchi za Kusini mwa Afrika kwa kuongeza wigo wa mapato kutokana na mizigo itakayoongeza katika upakuaji kwenye bandari ya Dar es Salaam.
Akizungumza na waandishi wa habari jana tarehe 17 Julai 2023, amesema zaidi ya asilimia 65 ya mizigo ambayo hushushwa katika Bandari ya Dar es Salaam hupita katika mpaka wa Tunduma kuelekea nchi za kusini mwa Afrika.
“Kupitia chanzo kimoja cha mapato cha magari makubwa yanayotoka bandarini kupitia mpaka wetu wa Tunduma tunakusanya Sh nane milioni mpaka 10 milioni kwa siku, Hivyo maboresho na uwekezaji wa DP World katika bandari yetu yatatusaidia kuongeza ukusanyaji wa mapato katika Mji wetu wa Tunduma,” alisema.
Alisema faida nyingine watakayoipata ni pamoja na kujenga bandari kavu katika mji wa Tunduma ambapo tayari walishatenga ekari 2000 kwa ajili ya uwekezaji huo.
“Tunawakaribisha wawekezaji wenye uwezo kuja kuwekeza katika eneo letu wawe wa ndani ya nchi yetu au kutoka nje bila kujali rangi, hata DP World tunawakaribisha kuwekeza Tunduma kujenga bandari kavu,” alisema.
Alisema Momba ni wanufaika wakubwa wa bandari ya Dar es Salaam, kupitia mapato ya ndani Halmashauri ya mji Tunduma imefanikiwa kuajiri watumishi 52 ambao wanalipwa kupitia mapato ya ndani.
Leave a comment