DAKTARI Muhammed Ali ambaye ni Mtanzania amefariki kwa ugonjwa wa Ebola nchini Uganda ambapo alikuwa akisomea shahada ya uzamili ya udaktari katika upasuaji. Anaripoti Mwandishi Wetu, Uganda … (endelea).
Ali mwenye umri wa miaka 37 ni miongoni mwa watu wanane waliothibitishwa na Serikali ya Uganda kufariki kwa Ebola huku watu 38 wakithibitshwa kuambukizwa.
Taarifa iliyotolewa leo Jumamosi Tarehe Mosi Oktoba, 2022 na Waziri wa Afya nchini Uganda, Jane Ruth Aceng imeeleza kuwa Ali amefariki dunia leo majira ya saa 9:13 alfajiri.
“Alipimwa na kubainika ni mwathirika wa virusi vya ebola Septemba 26, 2022 na amefariki alipokuwa akiendelea kupatiwa matibabu kituo cha Fort Portal RRH kilichotengwa kwa ajili ya wagonjwa wa ebola,” imeeleza taarifa hiyo.
Chama cha Madaktari wa Upasuaji nchini Uganga wametuma salamu za rambirambi kwenye kurasa zao za mtandao wa kijamii wa twitter.
Pia Waziri wa Afya nchini Tanzania, Ummy Mwalimu amenukuliwa na vyombo vya habari vya ndani akithibitisha kutokea kwa kifo cha Mtanzania huyo.
Mapema wiki hii wizara ya afya nchini humo ilisema kuwa wahudumu sita wa afya walipimwa na kukutwa na virusi vya Ebola ambapo inasemekana wengine waligusana na muathirika wa kwanza wa ebola.
Jana katika taarifa yake wizara nchini humo ilitangaza kuwa mlipuko wa Ebola ulikuwa umeenea katika wilaya nne.
Inaripotiwa kuwa watu wawili hadi sasa wamepona ugonjwa huo wa virusi vya Ebola vinavyotajwa kuwa adimu ambavyop hakuna chanjo yake.
Leave a comment