RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ametangazwa kuwa mshindi wa tuzo mbili za kimataifa na Jumuiya ya Kimataifa ya Watetezi na Amani. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Tuzo hizo ni Tuzo ya Amani duniani ya mwaka 2022 na tuzo ya Rais wa Dhahabu ya Malengo ya Maendeleo Endelevu ambayo ameweka rekodi ya kuwa Rais mwanamke wa kwanza kuipata barani Afrika.
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumamosi tarehe 1 Oktoba, 2022 na Mwenyekiti wa Taifa wa Umoja wa Wanawake wa CCM (UWT), Gaudencia Kabaka ambapo ameweka wazi kuwa tuzo hizo zitatolewa Oktoba 24 mwaka huu.
Amesema miongoni mwa mambo yaliyomfanya Rais Samia kupata tuzo hizo ni uboreshaji wa miundombinu ya afya na elimu ndani ya kipindi kifupi cha uongozi wake, utetezi wa masuala ya amani ikiwemo uhuru wa kuabudu na amani.
Mengine ni kujali masuala ya kijinsia kwa kuteua wanawake wengi katika uongozi, ujenzi wa madarasa katika shule za sekondari na msingi na utoaji wa elimu bila malipo.
“Wanawake wote wa Tanzania tumeona fahari sana kwa kuwa na Rais mwanamke ambaye ni Mheshimiwa Samia. Rais wa kwanza Afrika mwanamke kushinda tuzo mbili na kuandika historia ya kipekee nchini,” amesema.
Leave a comment