IMEELEZWA kuwa jumla ya Sh bilioni 1.5 zimetumika kujenga soko la kisasa la kuuzia samaki na dagaa litakalosaidia kuongeza mapato na kudhibiti upotevu wa mapato unaofanywa na baadhi ya wafanyabiashara wanaosafirisha bidhaa hizo kwenda nchini Zambia na Congo. Ibrahim Yassin, Songwe…(endelea).
Akizungumza jana tarehe 11 Februari 2023 Mwenyekiti wa halmashauri ya Tunduma, Ayoub Mlimba alisema kwa muda mrefu walikosa mapato kutokana na watu wengi kutunza samaki kwenye nyumba za watu zilizopo pembezoni mwa mpaka wa Tunduma na Zambia.
Alisema uwepo wa stoo hizo iliwalazimu wafanyabiashara kusafirisha hata usiku wa manane huku maafisa wa ukusanyaji ushuru wakishindwa kukusanya ushuru na kuikosesha mapato halmashauri na hata idara husika kushindwa kukusanya takwimu sahihi.
“Leo (jana) tunasaini mkataba kati ya mwenye eneo na halmashauri ambapo eneo la ekari 3.3 limechukuliwa na halmashauri itaikabidhi familia hii Sh milioni 30 pamoja na viwanja viwili vya makazi’’ alisema Mlimba.
Aidha, Mlimba alisema katika kipindi cha utawala wake mikataba yote itakuwa ikisainiwa eneo husika badala ya ofisini ili kuwepo na uwazi na kila mwenye malalamiko atoe ili kukwepa migogoro isiyokuwa ya lazima.
Afisa Uvuvi wa halmashauri ya mji huo, Elivathan Silwimba alisema sheria za uvuvi namba 22 ya mwaka 2003 na kanuni zake za mwaka 2009, inakataza kusafirisha mazao ya uvuvi saa 12 jioni kwa sababu kusafirisha muda huo hakuna anayechukua takwimu.
Alisema takwimu zilizokuwepo ni kwamba zilikusanywa kutokana na gunia 5000 za dagaa na gunia 2000 za samaki kwa mwaka.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya mji Tunduma, Philimon Magesa alisema ujenzi wa soko hilo kutaongeza chachu ya kiuchumi kwa serikali na mtu mmoja mmoja.
Alisema mradi utakapokamilika watajenga barabara zitakazolifanya eneo hilo la Chapwa kuchangamka kiuchumi kwani watu wengi watafungua biashara maeneo hayo wakiwemo mama lishe hivyo wanatarajia kuukamilisha mradi huo kwa wakati ili kuleta manufaa kwa wananchi.
Leave a comment