WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Innocent Bashungwa amewasimamisha kazi maofisa watano wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu mkoani Manyara ili kupisha uchunguzi kwa kusababishia Halmashauri hasara na matumizi mabaya ya madaraka. Anaripoti Apaikunda Mosha, TUDARCo … (endelea).
Watumishi hao ni Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Manunuzi, Juma Ibarahim Mavumo; aliyekuwa Kaimu mweka hazina, Ramadhani Mwakamyanda; Mweka hazina wa sasa, Respicius Kagaruki; Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA, Nyanda Komanya Msirikale na Mhasibu wa Mapato, David Assey.
Bashungwa amechukua hatua hiyo jana tarehe 27 Septemba, 2022 wakati akifanya majumuisho wa ziara ya kikazi ya kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu, Halmashauri ya Wilaya ya Hanang’ na Halmashauri ya Mji Mbulu, mkoani Manyara.
Bashungwa amesema tarehe 12 Julai 2022 aliyekuwa anakaimu ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya Mbulu, David Ali Assey aliandika barua kwa Kampuni binafsi ya kukopa kiasi cha shilingi milioni 6.7 kwa aijli ya matumizi ya ofisi na kuelekeza fedha hiyo kuwekwa kwenye akaunti binafsi ya Davidi ali Assey ambaye ni Mhasibu wa Halmashauri.
Amesema Taarifa ya CAG ya ukaguzi wa kawaida kwa mwaka wa fedha wa 2020/21 ilielekeza Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Manunuzi, Juma Ibrahim Mvumo achukuliwe hatua stahiki kwa kushindwa kuandaa vyema masharti ya zabuni na tangazo lake pamoja na kutofanya ufuatiliaji na uhakiki wa uhalali wa kampuni ya M/S Dicsamo Traders General Supplies Co. Ltd.
Bashungwa amesema aliyekuwa Kaimu Mweka Hazina, Ramadhani Mwakamyanda na weka Hazina wa sasa, Respicius Kagaruki wachukuliwe hatua kwa kulipa gharama za uwakala kwenye akaunti ya binafsi badala ya akaunti ya kampuni M/S Dicsamo Traders iliyopewa zabuni ya kukusanya mapato ndani ya Halmashauri kiasi cha shilingi 188,499,328.
Aidha, Amesema taarifa ya CAG ilielekeza Afisa TEHAMA wa Halmashauri, Nyanda Komanya na Mweka Hazina, Respicius Kagaruki wachukuliwe hatua kwa kushindwa kusimamia vyema Mfumo wa Mapato na kuacha mashine za kukusanyia mapato kuendelea kuwa nje ya mtandao kwa kipindi kirefu bila ufuatiliaji cha siku 8 hadi 1,051.
Wakati huo huo, ametoa wito kwa Mabaraza ya Madiwani kuacha tabia ya kukubali kutoa misamaha wa watumishi waliobainishwa kwenye taarifa ya CAG kuchuliwa hatua, na kubadilisha Maelezo hayo kutoa mapendekezo ya kuwapa onyo Watumishi hao.
Leave a comment