MAMLAKA ya usalama nchini Sudan imeripoti kuwa jaribio la mapinduzi lililofanywa leo asubuhi tarehe 21 Septemba 2021 na kundi la wanajeshi walioasi limetibuliwa na jeshi la ulinzi la nchi hiyo. Anaripoti Patricia Kighono, TURDACo … (endelea).
Katika hali isiyokuwa ya kawaida, televisheni ya taifa ya Sudan ilikatiza vipindi vyake na kutoa tangazo kwa umma kwamba wapinge jaribio hilo. Hata hivyo tangazo hilo halikufafanuliwa kwa kina.
Wakati huo huo, runinga hiyo ilianza kucheza nyimbo za kizalendo.
Aidha, taarifa iliyotolewa na mmoja wa wajumbe wa Baraza la Utawala la jeshi na raia nchini humo, Mohamed Al Faki Suleiman ameandika hivi kwenye mtandao wake wa Facebook; “Kila kitu kipo chini ya udhibiti… mapinduzi yaliyofanyika awalin ndio ushindi halali wa wasudani, tuyalinde.”
Mmoja wa maofisa wa jeshi la ulinzi la nchi hiyo amelieleza Shirika la Habari la Alkjazeera kwamba idadi isiyojulikana ya wanajeshi waasi kutoka kwenye kikosi cha vita walikuwa nyuma ya jaribio hilo na kwamba walitaka kuteka taasisi kadhaa za serikali lakini walizuiliwa na jeshi la nchi hiyo.
Ofisa huyo, ambaye hakutaka jina lake kwa sababu haruhusiwi kutoa taarifa kwa vyombo vya habari, amesema askari wengi, pamoja na maofisa wa ngazi za juu, wamekamatwa. Hakutoa maelezo zaidi, akisema kwamba taarifa ya jeshi itatolewa fupi baadae.
Sudan imekuwa na wakati mgumu kurejesha utawala wa kidemokrasia tangu jeshi kumfukuza mtawala wa muda mrefu wa nchini hiyo, Omar al-Bashir Aprili 2019, kutokana na maandamano ya miezi minne.
Nchi hiyo sasa inatawaliwa na serikali ya pamoja kati ya raia na jeshi lakini inakabiliwa na changamoto kubwa za kiuchumi na usalama.
Leave a comment