MHANDISI Mohamed Mtambo, aliyekuwa mgombea ubunge wa Mkuranga, Mkoa wa Pwani (ACT-Wazalendo), ameviomba vyama vya upinzania nchini Tanzania kuanza maandalizi mapema kwa ajili ya uchaguzi mkuu ujao ili kuindoa madarakani Chama Cha Mapinduzi (CCM). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Mtambo amesema hayo mwishoni mwa wiki, alipowapokea viongozi na wananchama wa Chadema, Kata ya Dondo, wilayani Mkuranga, ambao wamejiunga na ACT-Wazalendo.
Shughuli hiyo ya mapokezi ya wanachama wapya, ilifanyikia kijiji cha Mpafu akiwemo mwenyekiti wa Chadema, Kata ya Dondo, Abassi Ndambwe na aliyekuwa mgombea udiwani wa Chadema wa kata hiyo, Masudi Daruwishi.
“Tunataka mabadiliko ya kweli. Kwani tumezoea baada ya uchaguzi tunaondoka hatuonekani. Ili tuiondoe CCM madarakani, lazima tuanze kujipanga mapema na mimi nimerudi mapema kama mnavyoniona, ili tuanze kuijenga mapema Mkuranga yetu,” alisema Mtambo.
Aliwaomba wanachama hao wapya, kuanza kujipanga kwa ajili ya uchaguzi wa serikali za mitaa ili kujizolea vijiji na vitongoji vya kutosha “kwani ndugu zangu, tukiamua tunaweza. Twendeni pamoja, baba zangu, mama zangu, vijana wenzangu, nimerudi kuwashukuru kwa kura mlizonipa mwaka jana.”
Mhandisi Mtambo alisema, yupo tayari kushirikiana na wananchi wa Dondo katika kutatua changamoto mbalimbali.
Awali, Nurdin Mseti ambaye ni afisa wa chama hicho makao makuu, alisema “upinzani ni muhimu sanana sehemu ambayo wananchi walijaribu kuchgua upinzani maeneo hayo huwa hayarudi. Kwa maana hiyo, sisi hapa Mpafu na Dondo, tujiandae na tukijenge chama kweli kweli.”
“Mtambo hajaja kuugawa upinzani, hatuhitaji kugawana au kubomoana bali kujenga umoja imara ili tuweze kupata viongozi wa vitongoji na vijiji katika uchaguzi ujao wa serikali za mitaa,” alisema.
Kwa upande wake, Ndambwe alisema ujio wao ACT-Wazalendo ni kuimalisha upinzani ndani ya kata yao “na tutapiga kazi kweli kweli. Kata hii mimi naijua, sina shaka kabisa na Imani yangu tutaiondoa CCM.”
Akizunguza na wanachama hao wapya, Husna Sungura, aibu Katibu mwenezi ngome ya wanawake Taifa aliwaomba kuanza kujifunza na kufuatilia mambo ya ACT-Wazalendo.
“Msiwe wanyonge hata kidogo kwani lengo la chama chetu ni kuiondoa serikali madarakani. Wanawake tunaweza, tukiamua jambo letu hata wanaume wanaweza kutupa kura zao,” alisema.
Leave a comment