Naftaha Nachuma, Mbunge wa Mtwara Mjini (CUF) amedai, baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa, wameanzisha vikundi vya uhalifu kwa ajili ya kufanya fujo katika uchaguzi huo.
Nachuma ametoa madai hayo leo tarehe 4 Februari 2020, wakati akiuliza swali bungeni jijini Dodoma. Lililohoji mkakati wa serikali katika kukabiliana na changamoto ya uvunjifu wa amani kwenye uchaguzi huo.
Mbunge huyo wa CUF amemueleza Mhandisi Hamad Masauni, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, kwamba ana ushahidi juu ya swala hilo, na kumtaka aende Mtwara kuchukua ushahidi huo
“…pamoja na majibu mazuri nina maswali mawili , la kwanza hivi sasa Mtwara, Manispaa ya Mtwara Mikindani kuna baadhi ya viongozi wa siasa ambao wameweza kuratibu vikundi mbalimbali kwa ajili ya kufanya vurugu katika uchaguzi wa 2020, yuko tayari kuja Mtwara kuchukua ushahidi ambao nitampatia kwa mikono yangu,” amehoji Nachuma.
Akijibu swali hilo, Mhandisi Masauni amesema yuko tayari kuchukua ushahidi huo
“Swali lake la kwanza ameuliza kama niko tayari, niko kufanya hivyo kama ushahidi anao,” amejibu Mhandisi Masauni.
Wakati huo huo, Mhandisi Masauni amesema Serikali kupitia Jeshi la Polisi linanoa askari wake ili waweze kukabiliana na vitendo vinavyohatarisha usalama wa nchi kwenye uchaguzi mkuu unaotarajia kufanyika mwezi Oktoba mwaka 2020.
Mhandisi Masauni amesema kwa sasa askari hao wanapewa mafunzo ya ukakamavu na upelelezi, pia serikali imewaongezea vifaa vya utendaji kazi.
“Serikali kupitia Jeshi la Polisi inaendelea kutoa mafunzo mbalimbali ya kwa askari wake, ya ukakamuavu, upelezi na kuongeza vifaa vya kutendea kazi ili kuwajengea uwezo na ueledi mkubwa wa kuzuia na kukabiliana na vitendo hivyo vinavyojitokeza nyakati za uchaguzi,” amesema.
Leave a comment