JUMLA ya miradi 17 ya kimkakati katika mikoa ya Kanda ya Ziwa, yenye thamani ya Sh. 788 bilioni inaendelea kutekelezwa. Anaripoti Moses Mseti, Mwanza … (endelea).
Lengo la kutekelezwa kwa miradi hiyo ni kutatua kero ya muda mrefu ya maji, inayowakabili baadhi ya wananchi wa mikoa hiyo wanaotumia maji ya visima.
Kauli hiyo imetolewa na Prof. Kitila Mkumbo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji alipotembelea chanzo cha maji cha Nyahiti, likichopo Mapilinga wilayani Misungwi na baadaye kufanya mkutano wa hadhara kwenye eneo la Kisesa, Magu.
Miradi hiyo inatekelezwa na serikali kupitia Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira jijini Mwanza (Mwauwasa).
“Serikali inataka kumaliza kero ya maji na kuwa historia, inatekeleza miradi 17 ya kimkakati Kanda ya Ziwa kwa gharama ya shilingi bilioni 788 na itatumia maji ya ziwa hilo.
“Serikali imelivalia njuga tatizo la maji na sisi tutahakikisha linatatuliwa, hivyo mnapotuhukumu, angalieni tumetoka wapi na nini tunakifanya,” amesema Prof. Mkumbo.
Prof. Mkumbo amesema, wizara yake inatekeleza miradi mitatu katika Wilaya za Misungwi, Magu na Mji wa Lamadi wilayani Busega.
Pia amesema, kutokana na changamoto hiyo serikali imeanza kuchukua hatua za haraka kuhakikisha wananchi wa Kisesa, Bujora na Bukandwe wanapata maji ifikapo tarehe 15 Novemba mwaka huu, na miezi sita baadaye ujenzi wa tanki kubwa la maji utakuwa umekamilika.
“Kero ya maji ni kubwa na serikali hatua inazochukua kutatua kero hiyo si ahadi, inataka kupanua mtandao wa maji hapa Kisesa na kwingine ili kumaliza tatizo hilo kwa miaka mingi.,”alisema Profesa Mkumbo.
Leave a comment