OMBI la Kadinali Polycarp Pengo, Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam kung’atuka madarakani, limeridhiwa na Papa Francisko. Anaripoti Kelvin Mwaipungu … (endelea).
Papa Francisko amebariki ombi la Kadinali Pengo kuondoka madarakani alipokuwa kwenye maadhimisho ya Sherehe ya Bikira Maria Kupalizwa Mbinguni.
Hata hivyo, Papa Francisko amemteua Askofu mkuu mwandamizi, Yuda Thaddeus Ruwa’ichi wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam kuchukua nafasi ya Kadinali Pengo kuanzia sasa.
“Katika maadhimisho ya Sherehe ya Bikira Maria Kupalizwa Mbinguni, mwili na roho, tarehe 15 Agosti 2019, Baba Mtakatifu Francisko ameridhia ombi la Kardinali Polycarp Pengo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam, Tanzania la kung’atuka kutoka madarakani,” imeeleza taarifa ya Padre Charles Kitima, Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC).
Hivi karibuni, Kadinali Pengo katika maadhimisho ya kumbukumbu ya miaka 75 tangu kuzaliwa kwake, aliwaambia watu wa Mungu Jimbo Kuu la Dar es Salaam kwamba, anasubiria wakati wowote kumtii Baba Mtakatifu Francisko atakapomwambia kupumzika katika utume wa Kiaskofu.
Leave a comment