ALIYEKUWA Miss Tanzania mwaka 2006, Wema Sepetu amefungiwa kwa muda usiojulikana kujishughulisha na filamu na uigizaji, na Bodi ya Filamu Tanzania. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea)
Bodi ya Filamu imemtia kifungoni Wema kufuatia picha zake chafu zilizosambaa hivi karibuni kwenye mitandao ya kijamii, akiwa faragha na mwanamme anayedaiwa kuwa mume wake mtarajiwa.
Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu, Joyce Fisoo akizungumza na wanahabari baada ya kumhoji Wema leo tarehe 26 Oktoba 2018, amesema bodi hiyo imejiridhisha pasipo shaka kwamba Wema amelidhalilisha taifa, na kwamba kufuatia ukiukwaji huo imechukua hatua ya kumfungia.
Fisoo amesema licha ya adhabu hiyo, Bodi ya Filamu itafuatilia kwa karibu mwenendo wa Wema Sepetu na kwamba itamuondoa kifungoni itakapojiridhisha kuwa amejirekebisha.
“Wema amelidhalilisha taifa, kuwafanya watazamaji kuiga tabia, mwenendo, desturi na maadili yasiyo faa na wakiuke maadili yasiyokuwa ya kitanzania. Na kudhalilisha Tanzania kwa ujumla.
Kufuatia ukiukwaji huo imejiridhisha pasipo shaka na kuchukua hatua ya kumfungia Wema Sepetu kutojihusisha na masuala ya filamu na uigizaji hadi pale bodi itakapojiridhisha kwamba amejirekebisha, na itafuatilia kwa karibu mwenendo wake,” amesema na kuongeza Fisoo.
“Kufuatia kukiri makosa yake na kuomba radhi kwa maandishi kwa bodi ya filamu na watanzania kwa ujumla na kuonyesha kwamba anajutia kosa lake ni imani kwamba hatorudia.”
Leave a comment