RAIS John Magufuli amewataka wachezaji wa Timu ya Taifa ‘Taifa Stars’ kuifunga timu ya taifa ya Lesotho katika mchezo wa kuwania kufuzu kucheza michuano ya mataifa ya Afrika (AFCON) 2019 nchini Cameroon, unaotarajiwa kupigwa Novemba 18 2018. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Akizungumza na uongozi na wachezaji wa Taifa Stars leo tarehe 19 Oktoba 2018 Ikulu jijini Dar es Salaam, Rais Magufuli amesema timu hiyo ikifungwa itakuwa aibu na atajuta kuwaona kwa kuwa watu watasema amewapa mkosi.
“Lesotho mkifungwa itakuwa aibu nitajuta hata kuwaona, sababu mkifungwa watasema Magufuli amewapa mkosi wameenda kufungwa, vijana niwaombe msiende kufungwa. Tukiamua tutawapiga magoli mengi mno na wakija tuliocheza nao tutawatandika,” amesema Rais Magufuli.
Taifa Stars inatarajia kuifuata Lesotho tarehe 18 Novemba mwaka huu, ambapo inatakiwa kupata matokeo mazuri ili kujihakikishia tiketi ya kushiriki michuano ya AFCON inayotarajiwa kuanza kutimua vumbi mwakani nchini Cameroon.
Hadi sasa Taifa Stars iko nyuma ya Uganda kwa kushika nafasi ya pili katika kundi L, baada ya kufikisha pointi tano kufuatia matokeo ya bao 2-0 iliyopata dhidi ya Cape Verde kwenye mechi ya marudiano iliyochezwa Oktoba 16 2018 uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Leave a comment