RAIS John Magufuri ameichangia timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ kiasi cha Sh. 50 milioni kwa ajili ya maandalizi ya mchezo unaofuata dhidi ya Lesotho katika kuwania tiketi ya kufuzu kwa michuano ya kombe la Mataifa ya Afrika AFCON nchini Cameroon mwakani. Anaripoti Kelvin Mwaipungu … (endelea).
Rais Magufuli ametoa kiasi hicho cha pesa leo Ikulu alipokuwa akizungumza na wachezaji wa timu hiyo sambamba na viongozi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na Baraza la Michezo la Taifa (BMT) ili kutengeneza hamasa na timu iweze kufanya vizuri.
”Katika mechi yenu mnayokwenda kucheza nje na Lesotho nitawachangia Sh. 50 milioni lakini zitumike kwa wanaostahili ili hata posho za wachezaji ziongezeke,” amesema Rais Magufuli
Aidha Rais Magufuli alimtaka Waziri mwenye dhamana ya michezo nchini Dk. Harisson Mwakyembe kwa kushirikiana na TFF kuhakikisha timu inafuzu kwenye fainali hizo Mwakani nchini Cameroon maana italeta sifa kwa nchi sambamba na kujitangaza kimataifa.
”Rais Karia na Waziri Mwakyembe hakikisheni tunakwenda Cameroon 2019 ili mwisho wa siku mtengeneze historia kuwa mlikuwepo madarakani na Tanzania ilikwenda AFCON,” aliongezea Rais Magufuli.
Stars ambayo kwa sasa inashika nafasi ya pili kwenye kundi L baada ya kujikusanyia alama tano, inatarajia kucheza mchezo wake unaofuata dhidi ya Lesotho ambao utakuwa ugenini tarehe 18 Novemba, 2018 na kama itafanikiwa kushinda basi itakuwa imejiweka kwenye nafasi nzuri ya kufuzu.
Leave a comment