WENYEVITI wa mikoa ya chama kikuu cha upinzani nchini Tanzania- Chadema wamesema, kilichomtokea Lengai Ole Sabaya, aliyekuwa mkuu wa wilaya ya Hai, hakipaswi kuishia kwake kwani wapo wengi kama yeye mitaani wanaotakiwa kuchukuliwa hatua. Anaripoti Ibrahim Yamola, Dar es Salaam … (endelea).
Wametoa kauli hiyo leo Jumatatu, makao makuu ya Chadema, Kinondoni jijini Dar es Salaam, ikiwa ni siku chache zimepita tangu Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha kumhukumu Sabaya na wenzake wawili kifungo cha miaka 30 gerezani.
Ni baada ya kuwakuta na hatia katika kesi iliyokuwa inawakabili mahakamani hapo ya unyang’anyi wa kutumia silaha.
Akizungumza kwa niaba ya wenyeviti wenzake wa mikoa, Willium Mungai ambaye ni mwenyekiti wa mkoa wa Iringa amesema, kilichotokea kwa Sabaya ni funzo kwa wateuliwa kutotumia vibaya nafasi wanayopewa.
“Katiba ni muhimu ili akina Ole Sabaya wengine wasijitokeze, tumeona jinsi vyombo vilivyoshindwa kumchukulia hatua wakati hayo yakitokea kwani ndio wenyeviti wa kamati za ulinzi. Ndio maana Katiba ya Warioba ilikataa wakuu wa mikoa na wilaya wasiteuliwe ili kulinda maslahi ya wananchi na si ya mteule.”
Akisistiza hilo, Mungai amesema “wapo wengi akina Ole Sabaya, wanazunguka mitaani na tunaomba hao wengine waliobaki wachukuliwe hatua kwani wengine matendo yao yapo wazi.”
Mungai amewaomba wananchi wajitokezeni kuwataja na kutoa vithibitisho kwa vyombo vya dola ili waliobaki mitaani viwachukulie hatua na iwe funzo kwa wale wote wanaopewa dhamana.
Wenyeviti hao wamekutana kuzungumza na waandishi baada ya jana Jumapili kwenda gereza la Ukonga kumtembelea Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe.
Mbowe na wenzake watatu wanakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi yenye mashtaka ya ugaidi katika Mahakama Kuu, Divisheni ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, Dar es Sakaam.
“Tulikwenda kumtembelea mwenyekiti mwenzetu Freeman Mbowe na kumweleza sisi wenyeviti tupo pamoja naye na tutaendeleza juhudi za kupata Katiba mpya, tume huru ya uchaguzi na kupigania demokrasia,” amesema Mungai
“Leo ni siku ya 90 tangu Mbowe awe kizuizini. Tuwasihi wananchi keshokutwa 20 Oktoba, tujitokeze kwa wingi mahakamani kusikiliza uamuzi mdogo wa kesi hii muhimu kwa maslahi ya umma,” amesema
“Siasa ni uchumi, ukitaka uchumi ukue weka siasa safi, ukitaka jamii iendelee lazima kuwe na siasa safi na sasa tunamwomba DPP afute hii kesi kwani inachafua taswira ya taifa letu,” amesema
Aidha, wenyeviti hao wamesisitiza umuhimu wa katiba mpya ili kupunguza pia mamlaka ya Rais ikiwemo ya uteuzi ili kuwa na watumishi wa umma wenye weledi na si kuwa na viongozi “kama hawa kina Sabaya.”
“Wateule kama DC na RC wasiteuliwe moja kwa moja na Rais, wapitie bungeni kuthibitishwa au wananchi wawachague kwa kura za siri ili kuwa na viongozi wenye kuwatumikia wananchi si kama hivi tunavyoona haya yanayotendeka kama haya ya Sabaya yanayoumiza wananchi,” amesema Mungai
Wenyeviti hao wametumia fursa hiyo, kuwaomba wananchi kuendelea kujitokeza kujiandikisha kidijitali pamoja na kulipa ada za uanachama wa Chadema ambapo ada hizo hutumika kuendesha shughuli mbalimbali za chama.
Leave a comment