SERIKALI imetoa wito kwa wananchi kufuatilia taarifa za hali ya hewa ili kuwa na mipango sahihi katika shughuli za maendeleo. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Wito huo umetolewa leo tarehe 23 Machi 2022, na Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa katika maadhimisho ya siku ya Hali ya Hewa Duniani yaliyofanyika jijini Dar es Salaam.
Prof. Mbarawa amesema taarifa hizo zikitumika vizuri zitawawezesha wananchi kuelewa wakati gani sahihi wa kufanya shughuli fulani za kimaendeleo.
“Nawahimiza mzitumie vyema taarifa hizi kwa ajili ya kupanga vyema shughuli zenu mbalimbali za maendeleo na katika kufanya maamuzi sahihi kwa ustawi na maendeleo endelevu ya nchi yetu”, amesema Prof. Mbarawa.
Hata hivyo, amesema Serikali imeweka jitihada za makusudi za kuboresha Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini (TMA) kwa lengo la kuimarisha upatikanaji wa taarifa hizo za uhakika.
“Serikali itaendelea kuwekeza katika uboreshaji wa vifaa vya hali ya hewa kuwa vya kisasa zaidi ambapo kwa kufanya hivyo inazingatia pia mikataba ya kimataifa ikiwa ni pamoja na Mkataba wa Minamata kuhusu zebaki unaozitaka nchi zote duniani kuachana na matumizi ya vifaa vinavyotumia zebaki” amesema.
Waziri Mbarawa amesema TMA imefika kwenye kiwango cha kuridhisha ambapo imefikia kiwango cha asilimia 70 za kukubalika na Shirika la Hali ya Hewa Duniani.
Leave a comment