SHIRIKISHO la Mpira wa Miguu Duniani (FIFA) limesema uuzaji wa bia hautaruhusiwa ndani ya uwanja wakati mechi ikiwa inaendelea isipokuwa kwa masharti maalumu kwa watu watakaohudhuria mechi za Kombe la Dunia la FIFA nchini Qatar. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Taarifa iliyotolewa jana na FIFA imefafanua kuwa mashabiki walio na tiketi wataweza kununua bia wakati wa mechi, katika muda wa saa tatu kabla ya mechi na saa moja baada ya filimbi ya mwisho.
Qatar itawaruhusu watu wanaohudhuria mechi za kandanda za Kombe la Dunia, zitakazopigwa Novemba na Disemba mwaka huu nchini humo, kununua bia chini ya baadhi ya masharti hasa ikizingatiwa nchi hiyo ya kiislamu hairuhusu kunywa au kuuza pombe katika sehemu za wazi.
Ni mara ya kwanza kwa michuao ya Kombe la Dunia kufanyika katika nchi ya Kiislamu ambapo uuzaji wa pombe umedhibitiwa, jambo ambalo linaleta changamoto kubwa kwa waandaji, wakati michuano hiyo ikidhaminiwa na kampuni kubwa ya bia.
“Itawezekana kununua bia mara tu milango itafunguliwa, saa tatu kabla ya kuanza. Yeyote anayetaka kununua bia ataweza kufanya hivyo. (Mashabiki) pia wataweza kununua wakati wa saa moja baada ya kupulizwa kipenga cha mwisho,” imeeleza taarifa hiyo.
Budweiser, mmoja wa wafadhili wakubwa wa Kombe la Dunia, ataruhusiwa kuuza bia katika sehemu ya eneo kuu la mashabiki, lililoko katikati mwa Doha, kuanzia saa 6.30 jioni hadi saa saba usiku kila siku wakati wa mashindano, chanzo hicho kimesema.
Katika michuano ya Kombe la Dunia iliyopita, bia ilitolewa siku nzima katika “maeneo ya mashabiki”.
Leave a comment