WANANCHI wa vitongoji vilivyopo katika kata ya Mlowo halmashauri ya wilaya ya Mbozi mkoani Songwe wamechangia nguvu kazi kujenga shule ya sekondari Nambala kwa lengo la kupunguza msongamano wa wanafunzi kwenye shule mama ya Mlowo. Anaripoti Ibrahim Yassin, Songwe …(endelea).
Wakizungumza leo tarehe 2 Julai 2023 kwa nyakati tofauti, baadhi wakazi wa eneo hilo wakiongozwa na Safinia Mtafya, wamesema kutokana na umbali wa kilometa 10 wanaotumia watoto wao kwenda shule za Mlowo wameamua kujitolea nguvukazi kujenga shule.
“Watoto wetu wanapochaguliwa kujiunga kidato cha kwanza wanaenda kusoma shule zilizopo kata ya Mlowo wakitembea kilometa 10, kukamilika kwa shule hii itakuwa ni muarobaini wa kuongeza ufaulu na kuondokana na usumbufu wanaopata watoto wa kutembea umbali mrefu”amesema Mtafya.
Kaimu Afisa elimu sekondari wilayani humo Mwalimu Dorothy Mwandila amesema kutokana na changamoto ya ukosefu wa shule eneo hili, serikali imetoa Sh 470 milioni kujenga shule hiyo mpya.
Amesema halmashauri kupitia mapato ya ndani imetoa Sh 29.8 milioni, nguvu za wananchi Sh 2.5 milioni ambao pia walishiriki uchimbaji wa msingi ambao thamani yake ilikuwa Sh 800,000, uchotaji maji thamani yake 1.4, uchimbaji mashimo ya vyooSh. 360,000.
Pia wamepokea fedha Sh. 538.5 milioni kupitia mpango wa uboreshaji sekta ya elimu BOOST kujenga shule mpya Lutumbi yenye madarasa 14, jengo la utawala, madarasa ya awali ya mfano na vyoo matundu 18.
Katibu tawala mkoani Songwe, Happiness Seneda baada ya kutembelea shule hizo, ameeleza kuridhika na ujenzi huo huku akisisitiza kasi iongezwe ili wanafunzi waanze kusoma.
Leave a comment