Wananchi wa kijiji cha Mbembati kata ya Lubanda wilaya ya Ileje mkoani Songwe wamejenga zahanati ya Kijijini hapo kwa nguvu zao ili kupunguza adha ya kusafiri umbali wa kilomita nane kufuata huduma katika kituo cha afya Lubanda. Anaripoti Ibrahim Yassin, Songwe…(endelea).
Wananchi hao walianza ujenzi wa zahanati hiyo mwaka 2014 kwa lengo la kuwapunguzia akina mama wajawazito ambao walikuwa wakijifungulia njiani na majumbani wakati wakifuata huduma ya uzazi kituo cha afya Lubanda ambapo awali ilikuwa zahanati.
Akisoma taarifa ya kijiji, Mwenyekiti wa Kijiji hicho, Odeni Kandonga amesema kati ya fedha hizo wananchi wamechangia milioni 15.6, fedha ya mfuko wa jimbo ni milioni nne, na michango ya wahisani ni Sh 800,000.
Akijibu ombi la wananchi wa kijiji hicho Mkuu wa Wilaya hiyo, Farida Mgomi amewapongeza wananchi kwa kutumia nguvu zao kushiriki ujenzi huo kwa kuchangia fedha na kuahidi kuwa zahanati hiyo itakuwa ni mwarobaini wa kupata huduma za afya karibu pindi itakapoanza kutoa huduma
“Kutokana na mwitikio wenu Serikali itahakikisha inawaunga mkono kumalizia sehemu iliyobaki hivyo basi mhandisi wa ujenzi atakuja wiki ijayo kufanya tathmini ya eneo la zahanati ilipobaki ili jengo hilo liingizwe kwenye bajeti kwa ajili ya kutenga fedha za kukamilisha na huduma zianze kutolewa,” amesema Mgomi.
Leave a comment