WAFANYABIASHARA ndogondogo (wamachinga), katika eneo la Kivule jijini Dar es Salaam, wamemuomba Rais Samia Suluhu Hassan, awasaidie ili wapate mali zao zinazodaiwa kuchukuliwa na baadhi ya mgambo waliovunja vibanda vyao usiku wa kuamkia jana Jumanne. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Ombi hilo limetolewa na wafanyabiashara waliokumbwa na kadhia hiyo wakati wakizungumza na waandishi wa habari, jijini Dar es Salaam.
Wamedai kuwa, vibanda vyao vya biashara vimevunjwa kinyume cha sheria na baadhi ya viongozi wanaowalazimisha kwenda katika soko ambalo wanadai halina miundombinu mizuri ya wao kufanya biashara.
Mmoja kati ya wamachinga waliokumbwa na mkasa huo, Yusuph Mkuku, amesema “tunapenda kuiambia serikali kwamba kuna watu ambao wameanzisha soko lao kinyume cha sheria wametuma watu kuja kutuvunjia vibanda vyetu wakitulazimisha kwenda katika soko lao ambalo ili upate kizimba unatakiwa utoe Sh. 350,000 kwa mwezi.”
“Wanalitumia soko hilo kujinufaisha wenyewe lakini pia halina miundombinu mizuri ya kuvutia wateja kwanza ni chafu sana. Namuomba mama Samia atusaidie turudishiwe mali zetu mfano mimi nimeibiwa kuku 20 na waliochukua ni wale waliovunja vibanda,” amesema Mkuku.
Mwanaharakati huru, Bihimba Mpaya amewataka viongozi wa eneo hilo kutowasumbua wafanyabiashara ambao wamejitoa kwa ajili ya kutafuta ridhiki kihalali.
“Muda umefika sasa tunawataka walioiba mali zetu na tunawajua wako hapa KIvule, wazirudishe. Tunaita wezi kwa sababu hamuwezi kuvunja vibanda usiku bila sababu za msingi wakati vimejengwa katika maeneo sahihi,” amesema Bihimba.
Leave a comment