WANAJESHI wanne wakiwamo watatu kutoka Tanzania wamefariki dunia na wengine watatu pia Watanzania wamejeruhiwa katika shambulio la waasi lililotokea karibu na kambi yao huko Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC). Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Wanajeshi hao wanaunda Misheni ya Ulinzi wa Amani Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (SAMIDRC) ambayo ilipelekwa nchini humo kwa azimio la nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), kulinda amani na kurejesha utulivu mashariki mwa DRC.
Katika taarifa ya SAMIDRC ambayo imetolewa leo kwenye akaunti rasmi ya SADC katika mtandao wa X, imeeleza masikitiko ya taarifa ya vifo vya wanajeshi hao watatu wa Tanzania na mmoja kutoka Afrika Kusini.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa shambulizi hilo la kusikitisha limetokea baada ya kombora kurushwa kutua karibu na kambi waliyokuwa wakiishi wanajeshi hao.
“SAMIDRC pia inafahamisha umma kuhusu kufariki kwa mwanajeshi wa Afrika Kusini ambaye alifariki wakati akipatiwa matibabu kutokana na changamoto za kiafya katika Hospitali ya Goma, DRC,” imesema taarifa hiyo ambayo haikutaja muda wala siku ambayo shambulizi limetokea.
Wanajeshi hao walitumwa na nchi wa wanachama wa SADC kama sehemu ya msaada wa jumuiya hiyo kwenda kushughulikia masuala muhimu yanayoathiri utulivu na amani nchini humo kufuatia mapigano ya muda mrefu baina ya makundi ya waasi yenye silaha.
“Jumuiya ya SADC inatoa salamu za rambirambi kwa familia zilizopoteza wapendwa wao kutoka Tanzania na Afrika Kusini kwani ni hasara isiyoweza kuzuilika ya askari hawa waliokufa na wakati huo huo, inawatakia ahueni askari watatu waliojeruhiwa kupona haraka.
“SAMIDRC inaendelea kutekeleza majukumu yake kulingana na kanuni ya kujilinda kwa pamoja na hatua za pamoja zilizoainishwa katika Mkataba wa Ulinzi wa Pamoja wa SADC (2003),” imesema taarifa hiyo.
Leave a comment