BAADHI ya wabunge wameitaka Serikali ikamilishe mchakato wa kugawa majimbo, kata na tarafa zenye maeneo makubwa, ili kusogeza karibu na wananchi huduma za kiutawala. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Ombi hilo liliibuliwa leo tarehe 10 Novemba 2023, bungeni jijini Dodoma na Mbunge wa Manonga (CCM), Seif Gulamali aliyehoji “lini serikali itaugawa Mkoa wa Tabora na kupata mkoa mpya wa Manonga?
Baada ya Gulamali kuuliza swali hilo, Mbunge Viti Maalum, Tunza Malapo, aliuliza swali la nyongenza akihoji kwa nini Serikali isigawe majimbo yenye maeneo makubwa.
“lengo la kugawa maeneo ya utawala ni kurahisisha huduma kwa wananchi, lakini Tanzania kuna majimbo makubwa kama Mbeya Mjini na Tandahimba, Serikali ina mpango gani wa kuyagawa ili utoaji huduma kwa wananchi uwe rahisi?” alihoji Malapo.
Naye Mbunge wa Singida Mjini, Mussa Sima, aliiomba Serikali igawe kata zenye maeneo makubwa “kwa kuwa imefanyika sensa ya watu na makazi na ziko kata ni kubwa zinahitaji mgawanyo wake. Je nini mkakati wa Serikali katika kugawa kata hizo ili kufikisha huduma kwa wananchi?”
Akijibu maswali hayo, Naibu Waziri Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Dk. Festo Dugange, alitaka viongozi wa majimbo, kata na tarafa zenye maeneo makubwa, zifuate sheria za nchi zinazoshughulika na masuala ya ugawaji maeneo makubwa na uanzishwaji wa maeneo mapya.
“Serikali inatambua umuhimu wa kugawa maeneo, nashauri tuanze vikao vya kisheria kuanzia ngazi za vijiji, kata, mikoa na kisha kufikisha mapendekezo TAMISEMI na kuona uwezekanao wa kupata maeneo mapya,” alisema Dk. Dugange.
Leave a comment