VIONGOZI wa mashitaka nchini Uganda waliogoma wakidai ongezeko la mishahara wamekubali ombi la serikali la kurejea kazini huku wakati madai yao yakishughulikiwa, anaandika Catherine Kayombo.
Serikali iliwaomba viongozi hao miezi mitatu kushughulikia madai yao, na kuwaomba kurejea kazini ili kuepusha msongamano wa kesi nchini humo ingawa ombi hilo lilikataliwa awali.
Msemaji Mkuu wa muungano wa viongozi wa mashtaka, Awali Kizito, aliiwaambia wanahabari kuwa mkutano mkuu ndiyo utakaoamua kusitisha ama kuendelea na mgomo huo.
“Hatima ya mgomo wetu ipo mikononi mwa mkutano mkuu wa wanachama wetu, tunatarajia kukutana na kuamua ikiwa tutakubali ombi la serikali kusitisha mgomo huu au la”, alisema Kizito.
Viongozi hao waliokuwa wamegoma kwa takribani wiki moja, walikutana jana kuamua endapo wasitishe mgomo huo ambao umekwamisha kesi mahakamani.
Kufuatia mgomo huo, majaji wamekuwa wakiahirisha na kuchelewesha kesi kwa ukosefu wa waendesha mashtaka.
Moja ya kesi zilizocheleweshwa nchini humo ni ya mauaji ya aliyekuwa msemaji wa polisi, Andrew Felix Kaweso.
Leave a comment