BAADHI ya viongozi wa dini, wameiangukia Serikali wakiitaka ivunje mkataba iliyoingia na Serikali ya Dubai kupitia kampuni ya DP world kwa ajili ya kushirikiana kuendesha bandari nchini, kwa madai kuwa una athari katika uchumi wa nchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Pia wameitoa wito kuachia Watanzania wote waliokamatwa na vyombo vya dola kwa sababu za kukosoa mkataba huo.
Wito huo umetolewa leo Jumamosi, tarehe 23 Julai 2023, katika mkutano wa hadhara ulioandaliwa na wanaharakati kujadili athari za mkataba huo, uliofanyika jijini Dar es Salaam.
Mkuu wa Kanisa la Moravian la Uamsho Tanzania, Askofu Emmaus Mwamakula, amesema ni vyema mkataba huo ukavunjwa wakati huu kwa gharama ndogo, kuliko kuuvunja baadae kwa gharama kubwa.
“Viongozi wa dini tunajua zaidi kuhusu mkataba na siri iliyokuwepo ndiyo maana tunawatia ujasiri viongozi wengine kwamba Tanzania tunaweza kuondoka katika mkataba kwa gharama kidogo. Mnajua Djibout wameingia gharama kubwa sana. Kwa hiyo kuukatisha ni gharama ndogo,” amesema Askofu Mwamakula.
Katika hatua nyingine, Askofu Mwamakula, amewataka watu walioshiriki kuandaa mkataba huo, wauvunje mara moja ili kulinda heshima ya serikali.
“Hawa waliopokea hizi hela hizi kuingia kwenye mkataba wazitapike na Serikali iliyoko madarakani itaheshimika endapo itafanya vizuri katika huu mkataba,” amesema Askofu Mwamakula.
Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili, Amani na Haki za Binadamu kwa jamii ya madhehebu ya dini zote nchini, Askofu William Mwamalanga amesema katika kikao walichoketi viongozi wa dini hivi karibu wamemtuma kumuomba Rais Samia Suluhu Hassan aagize vyombo vya dola kuwaachia huru wote waliokamatwa kaa kukosoa mkataba huo.
Pia Mwamalanga wametoa siku tatu kwa genge lililomzingira Rais Samia kuutetea mkataba huo, kumuachia la sivyo viongozi hao wa dini watawataja hadharani.
Kwa upande wake Sheikh Mussa Kitima, amewataka wananchi waungane kwa pamoja katika kupaza sauti zao ili Serikali iache mpango wake wa kukodisha bandari.
Tangu mkataba huo wa ushirikiano wa kiserikali kati ya Tanzania na Dubai, kuhusu uwekezaji bandari nchini, uridhiwe na Bunge mwanzoni mwa Juni, 2023, makundi mbalimbali yameibuka wakiupinga kwa madai kuwa hauna maslahi kwa taifa.
Baadhi yao wanadai mkataba haujaonyesha ukomo wa muda wa utekekelezaji wake, maslahi ambayo nchi itapata kupitia uwekezaji husika na namna ajira za wazawa zitalindwa.
Hata hivyo, Serikali mara kadhaa imekanusha madai hayo ikisema huo sio mkataba wa biashara ndiyo maana haujaweka wazi masuala hayo na kwamba majibu ya maswali hayo yatajibiwa katika mikataba ya uwekezaji itakayoingia baadae, baada ya mkataba wa msingi kuridhiwa na pande zote mbili.
Leave a comment