MJUMBE wa Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), John Heche amemtaka Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Balozi na IGP(Mstaafu), Ernest Mangu atoke hadharani kwa ajili ya kuueleza umma msimamo wake kuhusu sakata la uwekezaji bandarini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Heche ametoa wito huo leo Jumamosi, akizungumza kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika wilayani Temeke, jijini Dar es Salaam.
“Sheria ya Bandari kifungu cha 6 inatambua Bodi ya Wakurugenzi ndiyo itakuwa wamiliki wa bandari kwa niaba yetu. Mwenyekiti wa bodi yupo, bodi ipo kama Hamza Johar kateuliwa na bodi kwenda kuwa muongoza timu ya majadiliano, baada ya kujadiliana inarudi. Mpaka sasa mwenyekiti hajatoka kuwaambia watanzania nini kimekubaliwa na nini msimamo wake kwenye hili,” amesema Heche.
Akizungumzia mkataba wa ushirikiano wa kiserikali kati ya Tanzania na Dubai, kuhusu uwekezaji wa bandari, Heche amesema una mapungufu makubwa kisheria, hivyo unatakiwa ufanyiwe marekebisho.
Naye Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Nyasa, Mchungaji Peter Msigwa, amewataka wananchi kuungana ili kuhakikisha mkataba huo haufanyi kazi kwa ajili ya kulinda maslahi ya taifa.
“Tunapokuja masuala ya kuokoa bandari matatizo makubwa zaidi, jambo hili linatakiwa kushirikiana kwa pamoja kuhakikisha tunalinda rasilimali zetu kwa ajili ya vizazi vijavyo. Sote tuungane tusikate tamaa kuhakikisha tunaokoa bandari zetu,” amesema Mchungaji Msigwa.
Leave a comment