MTANDAO wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), umetaka watu walioshambulia waandishi wa habari wa Kampuni ya Mwananchi Communication Ltd, wachukuliwe hatua za kisheria ili kitendo hicho kisifanywe tena. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Wito huo umetolewa leo Jumamosi na Mkuu wa Idara ya Huduma za Utetezi kwa watetezi wa haki za binadamu THRDC, Wakili Paul Kisabo, baada ya tukio hilo kutokea jana tarehe 22 Julai 2023, wakati wanahabari hao wanatekeleza majukumu yao kwenye Viwanja vya Buriaga, wilayani Temeke, Dar es Salaam.
Miongoni mwa wanaandishi hao ni, Fortune Francis, Sunday George, pamoja na dereva wa kampuni ya MCL, Omary Mhando, ambao wanadaiwa kujeruhiwa kwa kupigwa na kundi la vijana ambao halijafamika.
“Mtandao unatoa wito kwa wananchi kutoa ushirikiano kwa jeshi la Polisi ili wale wote waliohusika kuwashambulia waandishi hao wajulikane na wakamatwe kwa mujibu wa Sheria. Mtandao unatoa wito kwa jeshi la Polisi kufanya upelelezi kwa kuzingatia Sheria na Amri Kuu za Jeshi la Polisi (PGO), ili kuhakikisha kwamba wale wote waliohusika wanakamatwa na kufikishwa mahakamani kwa mujibu wa Sheria,” imesema taarifa ya Wakili Kisabo na kuongeza:
“Mtandao unatoa wito kwa wananchi kujiepusha na vitendo vya kuwashambulia waandishi wa habari ambao wamekuwa wakifanya kazi kubwa ya kuuhabarisha umma.”
Leave a comment