CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimegoma kutii agizo la Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, la kuahirisha kufanya mkutano uliolenga kuchambua mkataba wa ushirikiano wa kiserikali kati ya Serikali ya Tanzania na Dubai, kuhusu uendeshaji wa bandari nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Jana tarehe 22 Julai 2023, Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, Sisty Nyahoza, alikitaka chama hicho kuahirisha mkutano huo kwa madai kuwa unakiuka sheria za nchi kwa kuhusisha viongozi wa dini, kitendo kinachodaiwa kutumia udini katika kufikia malengo yake.
Pia, Nyahoza aliutaka uongozi wa Chadema, kufika ofisini kwake kesho Jumatatu, kwa ajili ya kujadili suala hilo na masuala mengine ya utekelezaji sheria za vyama vya siasa.
Naye Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe amesema “msajili anatuandikia barua anasema mnakwenda kuzungumza viongozi wa dini na taasisi nyingine. Aliyemuambia mkutano wa hadhara tunazungumza na wanachadema peke yake ni nani?”
“Mkutano wa Chadema tungekutana Mlimani City, lakini tunakutana Temeke uwanja wa hadhara ili tuzungumze na watanzania wote wa imani yote, tujadili nchi yetu ndiyo maana tulipuuza barua ile,” amesema Mbowe.
Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika, amesema mkutano huo haujaahirishwa kwa sababu barua ya msajili ilimfikia nje ya muda wa kazi “chama chetu kinafanya kazi kitaasisi kwa vikao, barua nikabaki nayo sababu tutakaa vikao vyetu vya chama niulize ule uamuzi ulikuwa sahihi au haukuwa sahihi.”
Kuhusu wito wa kufika kwa msajili, Mnyika amesema Chadema hakitaitikia wito huo kwa kuwa wanachama wake wameshauri hivyo.
“Kwa sababu sisi ni chama kinachosikiliza umma na sauti ya watu ni ya Mungu, hatutakwenda kesho kuonana na msajili ,” amesema Mnyika.
Mkutano huo umefanyika leo Jumapili, katika mkutano wa Bulyaga, Dar es Salaam na kuhudhuriwa na baadhi ya viongozi wa dini mbalimbali.
Leave a comment