NCHI ya Urusi, imeonya uwezekano wa dunia kukumbwa na baa la njaa, endapo vikwazo vya kiuchumi dhidi yake havitaondolewa haraka iwezekanavyo. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Tahadhari hiyo imetolewa leo Ijumaa, tarehe 15 Apriuli 2022 na Naibu Mwenyekiti wa Kamati ya Baraza la Shirikisho la Mambo ya Nje Urusi, Andrey Klimov, katika mkutano wake na waandishi wa habari wa Afrika, uliofanyika kwa njia ya mtandao.
Klimov amesema, Urusi ambayo ni wazalishaji na wasambazaji wakubwa duniani wa mafuta, ngano, gesi , wamewekewa vikwazo vya kiychumi na usafirishaji, ambavyo vinasababisha washindwe kusambaza bidhaa hizo muhimu katika nchi wahitaji, hasa za Afrika, Asia na Amerika ya Kusini.
“Bandari ya Urusi tunayotumia kusambazia chakula kuleta kwenu, kupitia Bahari ya Mediterranean imefungwa, hatuwezi kusambaza. Vikwazo hivi vilivyo kinyume cha sheria havidhuru Urusi, tuna usalama wa kutosha. Lakini inatishia Afrika na nchi nyingine ambazo hazina usalama wa chakula,” amesema Klimov.
Aidha, Klimov amesema, kwa kuwa nchi yake imewekewa vikwazo katika matumizi ya mifumo ya kifedha duniani, nchi za Afrika zinaweza kununua bidhaa zake kwa kutumia fedha yake, Rubble.
“Mnaweza kufikiria jinsi Urusi ilivyopigwa marufuku kufanya miamala, Afrika inaweza kufanya miamala kwa kutumia Rubble,” amesema Klimov.
Urusi imewekewa vikwazo vya kiuchumi, kidiplomasia na kijamii na mataifa ya nje kufuatia msimamo wake wa kuivamia kijeshi Ukraine, mwishoni mwa Februari 2022.
Vikwazo dhidi ya Urusi, vimesababisha mfumuko wa bei ya bidhaa muhimu duniani, ikiwemo mafuta, mbolea na ngano, kitendo kinachopelekea Serikali nyingi duniani, ikiwemo ya Tanzania, kuja na mikakati ya kukabiliana na athari hizo.
Miongoni mwa sababu zinazotajwa na Urusi kuanzisha mapigano ya kijeshi Ukraine, ni kulinda maslahi ya nchi yake.
Leave a comment