HATIMAYE kata ya Kilimani katika Jiji la Dodoma imeanza ujenzi wa shule ya msingi itakayogharimu kiasi cha Sh 80 milioni kwa kuanza na vyumba vinne vya madarasa. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…(endelea).
Ujenzi huo wa shule ya msingi unatokana na kata hiyo kutokuwa na shule ya msingi wala sekondari tangu kupatikana kwa Uhuru wa Tanganyika.
Hali hiyo inatajwa kusababisha watoto kutembea umbali wa kilomita tatu kusaka elimu katika vijiji jirani.
Hata hivyo, leo tarehe 11 Oktoba 2023 Viongozi wa Kamati ya siasa ya Chama Cha Mapinduzi Kata ya Kilimani Jijini Dodoma pamoja na Wajumbe wa Sekretarieti ya kata ya kilimani wamefanya ziara ya kukagua mradi wa ujenzi wa Shule ya Msingi unaotekelezwa katika Mtaa wa Chinyoyo.
Pamoja na kasi ya ujenzi huo unaoendelea viongozi hao wamesisitiza kasi katika ujenzi huo ili ukamilike kwa haraka na kwa wakati.
Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi kata ya kilimani, Nathani Chibeye amesema ujenzi huo wa shule ya msingi utakuwa mkombozi kwa kata ya kilimani na kuondoa adha ya watoto kutembea umbali mrefu kwenda shule za jirani.
Kwa upande wake Katibu wa CCM kata ya Kilimani, Rotta Ndimbo ameitaka kamati ya ujenzi na mkandarasi kuhakikisha wanatanguliza uzalendo katika ujenzi wa shule hiyo ili thamani ya fedha zilizotengwa kwa ajili ya ujenzi huo zitumike kama zilivyo kusudiwa.
Leave a comment