RAIS mstaafu, Dk. Jakaya Kikwete, ameshauri fedha zinazotengwa katika bajeti za serikali, zitumike vizuri ili zilete tija. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Dk. Kikwete ameyasema hayo leo tarehe 22 Novemba 2023, jijini Dodoma, akizungumza katika mkutano wa nne wa maendeleo ya biashara na uchumi.
Ni siku chache baada ya majadala wa ubadhirifu wa fedha za umma uliobainishwa katika ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG),kutikisa Bunge, ambapo baadhi ya wabunge walishauri wabadhirifu wanyongwe.
“Hakikisheni mnatumia vizuri pesa kidogo mnazopata, maana kilichojitokeza wakati mwingine tunalalamika kuhusu bajeti lakini hata zile tulizopewa matumizi yake sio mazuri.”
Katika hatua nyingine, Dk. Kikwete amesema ili uchumi wa nchi yeyote ukue, inabidi Serikali iboreshe mazingira ya uwekezaji “hakuna uchumi utakaokuwa lakini hupendi wawekezaji. Lakini uwekezaji unastawi pale ambapo mazingira ni rafiki.”
Akizungumzia kongamano hilo, Rais Kikwete ameishauri washiriki wake kulitumia katika kupata ushirikiano wa kufanya tafiti zitakazoleta majawabu ya matatizo yanayokabili jamii.
“Kongamano kama hili linaleta fursa kuibua mtazamo mpya na mbinu mpya katika kutatua changamoto zinazoikabili jamii,” amesema Dk. Kikwete.
Katika hatua nyingine, Dk. Kikwete amesema Rais anapoingia madarakani sio kwamba anajua kila kitu, ndiyo maana anakuwa na washauri pamoja na wasaidizi kama mawaziri na makatibu wakuu, ambao wanampa ushauri.
“Unapoingia hujui kitu…lakini ukiwa Rais unatakiwa ushughulike na kila jambo. Kwa sababu huwezi kujua kila jambo lazima utegemee sana ushauri ndio maana Rais ana mawaziri, manaibu mawaziri, makatibu wakuu, makamishna na wakurugenzi. Pale Ikulu ana ofisi binafsi ina mabingwa wa kumshauri,” amesema Dk. Kikwete.
Dk. Kikwete amesema “ukikosa ushauri mzuri au ukipata ushauri mzuri lakini ukaupuuza hiyo nchi itakwenda kusikotakiwa kwenda. Ndiyo maana makongamano kama haya ni muhimu sana yanatoa mawazo yanayoisaidia serikali kuendesha nchi vizuri.”
Leave a comment