MTANDAO wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania(THRDC), umezindua mpango mkakati wake wa miaka mitano (2023-2027), unaotarajia kugharimu kiasi cha Sh. 46.1 bilioni kwa ajili ya kuimarisha haki za binadamu nchini. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Mpango mkakati huo umezinduliwa hivi karibuni jijini Dar es Salaam, ambao umejikita katika maeneo matatu, ambayo ni ulinzi na usalama wa watetezi wa haki za binadamu.
Usimamizi wa wanachama wake na ushiriki wa jamii, katika utetezi na la mwisho ni uendelezaji wa taasisi.
Akizungumza baada ya uzinduzi huo kufanyika, Mratibu wa THRDC, Onesmo Olengurumwa, alisema mkakati huo utasaidia kuimarisha haki za binadamu, ikiwemo maslahi na usalama wa watetezi wake.
“Mkakati umejikita maeneo makubwa mfano maeneo tunajaribu kuzingatia zaidi katika kipindi cha miaka mitano, kuhakikisha kwamba watetezi wa haki za binadamu wanapata kikamilifu ule uhuru wao wa kufanya kazi za utetezi. Nyie ni mashahidi kwamba miaka mitano iliyopita hali ilikuwa tete na mazingira yalikuwa magumu,” alisema Olengurumwa.
Mratibu huo wa THRDC, alisema kupitia mkakati huo mtandao utahakikisha mazingira ya kisera na kisheria kwa taasisi zinazosimamia masuala ya haki ili zifanye kazi zao kwa uhuru.
“Kingine kuendelea kuwa na mikakati ya ushirikishwaji na ushirikishaji kwa kufanya kazi kwa pamoja na wadau mbalimbali ikiwemo Serikali. Mmeona kwa namna gani mwaka huu tumeanza mikakati ya kufanya kazi na Serikali,” alisema Olengurumwa na kuongeza:
“Serikali iliyoingia madarakani ya Rais Samia Suluhu Hassan, tuliona imeanza kujipambanua ni Serikali yenye lugha nzuri kwenye haki za binadamu. Tunataka tutumie fursa iliyopo tuweze kufanya maboresho katika sekta zinazohusu uhuru wa haki za binadamu, nafasi ya kiraia ya kujadili mambo ya kitaifa.”
Kwa upande wake Mrajisi wa Asasi za Kiraia Zanzibar, Ahmed Khalid Abdullah, aliipongeza THRDC kwa kuandaa mkakati huo akisema uatsaidia kuzijengea uwezo asasi katika utekelezaji wa shughuli zake.
“THRDC imeweza kutusaidia sana hasa katika suala zima la kutujengea uwezo, wameanza kufanya kazi na Mahakama Kuu lakini wameingia katika Tume ya Marekebisho ya Sheria. Lakini mpango wetu kuangalia asasi ndogo za Zanzibar ili ziweze kuwa na nguvu ya kukamilika kwa yale malengo yao,” alisema Abdullah.
Leave a comment