MTANDAO wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), umesaini mkataba wa mwaka mmoja wenye thamani ya Dola za Kimarekani 70,000 (Sh. 175,000,000 na Shirika la American Bar Association kutoka nchini Marekani. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na THRDC, mkataba huo ni sehemu ya miradi ya ABA kuhusu masuala ya uhuru wa kujieleza ili kuboresha hali ya Watetezi wa Haki za Binadamu nchini.
“Makubaliano hayo yamesainiwa rasmi tarehe 11 Aprili 2024 na utekelezaji wake utaanza rasmi mwishoni mwezi huu na kumalizika tarehe 31 Mei 31 2025. Fedha hizi zitatumika kutekeleza lengo kuu la mradi ambalo ni kuhamasisha uhuru wa kujieleza nchini pamoja na malengo mengine maalumu,” imesema taarifa ya THRDC.
Malengo mengine ni kuimarisha uwezo na ushirikiano wa vyombo vya habari, asasi za kiraia na wadau wa sekta ya kisheria katika kudai haki ya kujieleza kwa uhuru.
Lengo lingine ni kuongeza uelewa na uungaji mkono wa wapangaji sera kwa sera na mifumo ya kisheria inayothibitisha demokrasia kwa kuthamini uhuru wa kujieleza.
THRDC imesema wanufaika wa mradi huo watakuwa watetezi wa haki za binadamu, ikiwemo waandishi na wamiliki wa vyombo vya habari, walinzi wa haki za binadamu, mashirika ya kiraia na makundi mengineyo ya utetezi wa haki za binadamu.
Shirika la American Bar Association, limekuwa likishirikiana THRDC tangu 2020 katika kutekeleza miradi mbalimbali ya mtandao, wakiwa ni Wadau wakubwa wa Haki za Binadamu nchini Tanzania.
Leave a comment