UMOJA wa Vijana wa unaojitanabaisha kwa jina la ‘Team Wazalendo’ umesema kuwa utachukua jukumu la kuuelimisha umma juu ya umuhimu wa uwekezaji katika bandari ya Dar es Salaam na kuisisitiza Serikali kutorudi nyuma katika mradi huo lakini pia iendelee kutafuta wawekezaji wengine katika bandari nyingine. Anaripoti Maryam Mudhihir …(endelea).
Hayo yamesemwa na Frank Rugwana aliyejitambulisha kuwa ni Mwenyekiti wa umoja huo leo tarehe 17 Julai 2023, jijini Dar es Salaam, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.
Rugwana ameeleza kuwa uwekezaji huo katika bandari ya Dar es Salaam unafaida hasa ikizingatiwa kampuni ya DP World ina uzoefu mkubwa utakaoweza kuiongozea bandari ya Dar es Salaam mnyororo wa thamani katika sekta ya usafirishaji duniani.
Amesema kuwa yeye na wenzake wanaungana mkono Serikali kwa kuanzisha makubaliano ya awali katika uwekezaji bandarini na kampuni ya DP World (IGA) kwa matarajio ya ufanisi wa kuharakisha upakuaji wa mizigo bandarini.
“Hapo awali ilikuwa unatumia mpaka wiki tatu kutoa mzigo bandarini lakini baada ya DP kusimika mifumo yao ndani ya saa moja baada ya kulipa utapata mzigo wako.
“Uwekezaji huu utapunguza kero za kusubiri mizigo kwa siku tatu kunasababisha ukuaji wa uchumi kuwa mdogo”, amesema Rugwana.
Rugwana anasema kuwa uwekezaji katika bandari hiyo ni fursa pekee ya kiuchumi kwani inaweza kuchangia mpaka asilimia 67 ya bajeti yote ya serikali ambapo kwa sasa inachangia asilimia 35 ya bajeti.
Rugwana ameishauri serikali kuendelea kutafuta wa wekezaji wengine wenye uwezo na ujuzi ili kuendelea kupata fursa mbalimbali zilizopo nchini.
Rugwana na wenzake wanasisitiza kuwa wao ni wazalendo wasiotokana na chama chochote cha siasa wao wanasimama kwa ajili ya maendeleo ya nchi.
Leave a comment