WAKATI tunaadhimisha miaka mitatu madarakani ya Rais Samia Suluhu Hassan, Wakala wa Barabara Tanzania (TANROAD), mkoa wa Morogoro, umefanikiwa kutekeleza miradi miwili mikubwa ya ujenzi wa barabara za lami na kusaini mikataba mipya minne. Anaripoti Victor Makinda, Morogoro … (endelea).
Akizungumzia mafanikio ya TANROAD mkoa wa Morogoro kwa kipindi cha miaka mitatu ya Rais Samia, Meneja wa TANROAD mkoa wa Morogroro, Mhandisi Razack Kyamba anasema kuwa Rais Samia ameonesha dhamira ya dhati kuhakikisha tatizo la miundombinu ya barabara mkoani Morogoro linapatiwa ufumbuzi wa kudumu.
Mhandisi Kyamba anasema ipo miradi ya ujenzi wa barabara ambayo tayari imekamilika huku TANROAD ikiwa imesaini mikataba mingine mikubwa ya ujenzi wa barabara muhimu zinazounganisha wilaya za mkoa wa Morogoro ambapo kukamilika kwake kutachochea kasi ya ukuaji wa uchumi na ustawi wa jamii.
“Katika kipindi cha miaka mitatu ya Rais Samia, TANROAD Morogoro imetekeleza mradi wa barabara ya lami kutoka Rudewa mpaka Kilosa mjini barabara yenye urefu wa Kilometa 24 na madaraja matatu ambapo jumla ya Sh 32.9 bilioni zimetumika, mradi huo tayari umekamilika” Anasema Mhandisi Kyamba.
Mhandisi Kyamba anautaja mradi mwingine unaotekelezwa na TANROAD mkoa wa Morogoro kuwa ni mradi wa ujenzi wa barabara ya lami yenye urefu wa Kilometa 66.9 kutoka Kidatu mpaka Ifakara wilayani Kilombero uliogharimu Sh 104 bilioni.
Anasema kuwa mradi huo upo kwenye hatua za mwisho kukamilika ambapo kukamilika kwake kutakuwa chachu kubwa ya kukuza uchumi wa wananchi wa wilaya ya Kilombero inayokaliwa na wakazi wengi ambao ni wakulima wazalishaji wakubwa wa zao la mpunga, miwa na mazao mengine ya biashara na chakula.
Anaongeza kuwa mradi wa barabara ya Kidatu Ifakara una umuhimu mkubwa katika kukuza shughuli za utalii kwa kuwa barabara hiyo inapita pembezoni mwa Hifadhi ya Milima ya Udzungwa.
Mhandisi Kyamba anasema kuwa katika mwaka huu wa fedha, TANROAD mkoa wa Morogoro imesaini mikataba mipya minne ya ujenzi wa barabara za lami ambazo ni muhimu kwa ukuaji wa uchumi wa watu wa Mkoa wa Morogoro na Taifa kwa ujumla.
“Tumekwisha saini mkataba ya ujenzi wa barabara ya kutoka Ifakara kwenda Mbingu, wilayani Kilombero barabara yenye urefu wa Kilometa 62.5 tayari mkandarasi HEGO amekwisha anza kazi.
Sambamba na ujenzi wa barabara hiyo hiyo kutoka Mbingu kwenda Chita Kilometa 37.5 ambapo pia mkataba umekwisha sainiwa,” anasema Mhandisi Kyamba.
Anautaja mkataba mwingine wa ujenzi wa barabara uliokwisha sainiwa ni barabara ya kutoka Bigwa mpaka Kisaki kilometa 78 Wilaya ya Morogoro.
“Upo mkataba mwingine wa ujezi wa barabara ya kutoka Ubena Zomozi kwenda Ngerengere Kilometa 10 ambao tayari umesainiwa na mkandarasi anatarajia kuanza kazi hivi karibuni.”
Mhandisi Kyamba anasema kuwa sambamba na ujenzi wa barabara hizo za lami TANROAD Morogoro inatarajia kutekeleza mradi wa ujenzi wa madaraja korofi ambayo hufurika maji wakati wa masika na kupelekea wananchi kushindwa kuvuka ambayo ni daraja la Nguyani na Chakwale yaliyopo wilayani Gairo.
Anasema kuwa Rais Samia amekwisha ridhia ujenzi wa madaraja hayo muhimu na tayari kibali cha ujenzi kimetoka, zabuni za ujenzi huo itatangazwa hivi karibuni na atakapo patikana mkandarasi ujenzi utaanza mara moja.
Mhandisi Kyamba anasema kuwa TANROAD mkoa wa Morogoro illipokea maelekezo ya serikali ya kujenga barabra za kuingia kwenye kituo cha treni ya Mwendokasi (SGR) mkoa wa Morogoro.
Katika kutekeleza agizo hilo wakala huo upo katika hatua za mwisho za kusaini mkataba kwa kuwa zabuni za ujenzi wa barabara za lami kuingia stesheni hiyo zilikwisha tangazwa.
“Ujenzi wa barabara ya kuingia stesheni ya treni ya mwendokasi mkoa wa Morogoro yenye jumla ya Kilometa 13 unatarajiwa kuanza hivi karibuni tukitarajia kuwa ujenzi huo utarahisisha abiria na mizigo kuingia na kutoka stesheni hapo,“ anasema Mhandisi Kyamba.
Mhandishi Kyamba anasema kuwa TANROAD mkoa wa Morogoro inampongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa uongozi wake ulitukuka unaojali maslahi ya wananchi na wao TANROAD watazidi kumuunga mkono kwa kutekeleza wajibu wao kwa weledi, bidii na maarifa.
“Tanroads mkoa wa Morogoro tutandelea kusimamia miradi yote ya ujenzi wa barabara na tuko tayari wakati wote kupokea maagizo ya serikali na kuyatekeleza kwa viwango stahiki ili kwa pamoja tuendelee kuiunga mkono dhamira njema ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kuwaletea maendeleo wananchi,” anasema Mhandisi Razack Kyamba.
Leave a comment