MBUNGE wa Simanjiro (CCM), Christopher Ole Sendeka, ameelezea namna watu wasiojulikana walivyoshambulia kwa risasi gari lake akiwa njiani kurudi jimboni kwake, akisema kabla hawajafanya tukio hilo walikuwa wanamfuatilia kwa nyuma. Anaripoti Mwandishi Wetu. Dar es Salaam…(endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari saa chache baada ya tukio hilo kutokea jana Ijumaa, Ole Sendeka alidai baada ya kuona gari la watu hao wasiojulikana linawafuatilia kwa nyuma, waliamua kulipisha lakini baada ya kufika katika usawa wao upande wa kulia walianza kuwamiminia risasi kwa mbele.
“Ilikuwa majira ya saa 1 kasoro usiku, kuna gari ilikuwa inatufuatilia kwa nyuma na ikaja tukawa kama tunataka kuwapisha wapiti kulia walipofika usawa wetu wakaanza kumimina risasi kwa dereva baada ya hapo wakavuta kwenda mbele halafu wakaanza kupiga risasi za usoni na sisi tukakata kona kugeuza name nikapiga za juu pale kuwatisha ndio tukafanikiwa kugeuza na kuondoka na wao wakaondoa,” alisema Ole Sendeka.
Mbunge huyo wa CCM alidai kuwa, watu hao walikuwa wanatumia silaha ndogo na kubwa. Alipoulizwa kama alifanikiwa kuona sura zao au namba za gari walizokuwa wanatumia, alidai hakufanikiwa kuziona.
“Hakuna aliyepata madhara na ndani ya gari tulikuwa mimi na dereva wangu, kutokana na purukushani zilizokuwepo hatujatambua sura wala namba za gari lililohusika na wala sijui kwa wakati huu sababu za hao watu kufanya tukio hilo,” alidai Ole Sendeka.
Tukio hilo linadaiwa kutokea jana wakati Ole Sendeka anarudi jimboni kwake kupitia njia ya Kiteto, ambapo gari aina ya Double Cabin Silver iliwafuatilia na baadae kuanza kuwafyatulia risasi kadhaa zilizoishia katika gari na kushindwa kuwaathiri waliokuwamo ndani.
Tayari Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini, David Misime, amesema wametuma timu ya watalaamu wa uchunguzi kwa ajili kubaini waliohusika.
Leave a comment