HATIMAYE Wizara Ofisi ya Rais-TAMISEMI, imetoa taarifa rasmi kuhusu hali ya kiafya ya Naibu Waziri wake, Dk. Festo Dugange, aliyepata ajali jijini Dodoma, usiku wa tarehe 26 Aprili 2023. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
TAMISEMI imetoa taarifa juu ya hali ya Dk. Dugange, ikiwa zimepita takribani siku mbili, tangu apate ajali ambapo awali wahusika wa Wizara hiyo walisita kutoa taarifa juu ya ajali hiyo licha ya kupigiwa simu na baadhi ya vyombo vya habari ikiwemo MwanaHALISI Online.
Leo tarehe 29 Aprili 2023, TAMISEMI imetoa taarifa kwa umma ikisema Dk. Dugange anapatiwa matibabu katika Hospitali ya Benjamin Mkapa, jijini Dodoma, kutokana na majeraha aliyoyapata katika ajali hiyo na kwamba anaendelea vizuri kiafya.
Taarifa hiyo imesema kuwa, Makamu wa Rais, Dk. Phillip Mpango, amefika hospitalini hapo kumjulia Hali.
“Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip I. Mpango akizungumza na Naibu Waziri Ofisi ya Rais TAMISEMI, Dkt. Festo Dugange leo tarehe 29 Aprili 2023 wakati alipofika hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Benjamin Mkapa kumjulia hali baada ya kupata ajali ya gari,” imesema taarifa hiyo na kuongeza:
“Dk. Dugange alipata ajali usiku wa tarehe 26 Aprili 2023 wakati akiendesha gari yake binafsi Jijini Dodoma ambapo kwa sasa anaendelea kupatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Benjamini Mkapa.”
Taarifa hiyo ya TAMISEMI imekuja kufuatia maswali yaliyoibuliwa na baadhi ya watu mitandaoni juu ya usiri wa ajali hiyo iliyomfika Dk. Dugange.
Kabla ya taarifa hiyo kutoka, MwanaHALISI Online ilimtafuta Afisa Habari wa TAMISEMI, Nteghenjwa Hossea kutaka uthibitisho wa ajali hiyo, lakini alijibu akitaka Mwandishi amtafute Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Adolf Ndunguru.
Ndunguru alipotafutwa naye alimuelekeza Mwandishi amtafute Waziri Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Anjella Kairuki ambaye naye hakupokea simu.
Leave a comment