ALIYEKUWA Waziri wa fedha wa Uingereza, Rishi Sunak ameimarisha nafasi yake ya kuweza kuchaguliwa kuwa waziri mkuu mpya wa Uingereza, baada ya kuongoza tena katika kura iliyopigwa na wabunge wa chama chake cha Conservative katika mbio za kurithi mikoba ya Boris Johnson aliyejiuzulu. Inaripoti Mitandao ya kimataifa… (endelea).
Katika kura hiyo iliyopigwa usiku wa kuamkia leo tarehe 19 Julai, 2022, Sunak aliungwa mkono na wabunge 115, akifuatiwa na waziri wa zamani wa ulinzi, Penny Mordaunt aliyechaguliwa na wabunge 82.
Waziri wa mambo ya nje, Liz Truss amekuja katika nafasi ya tatu kwa kupata kura 71, naye Kemi Badenoch alimudu kura 58 na kufanikiwa kubaki katika mchuano huo.
Tom Tugendhat aliambulia kura 31 na hivyo kuenguliwa, na kubakisha watia nia wanne tu katika kinyang’anyiro hicho.
Wawili watakaosalia baada ya duru nyingine ya mtoano bungeni, watapigiwa kura na wanachama wa Conservative na mshindi atakuwa waziri mkuu mpya wa Uingereza.
Leave a comment