SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) imesema, itahakikisha wananchi wanakuza uchumi wa kisasa unaoendana na falsafa ya uchumi wa kidijitali na uchumi wa bluu kwa kutumia teknolojia ya habari na mawasiliano (Tehama). Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea).
Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi wa Zanzibar, Amoul Hamil wakati akikabidhi kituo cha Kompyuta kwa Umma (Tele-Center) kwa Shule ya Sekondari Tumbatu.
Kituo hicho kimejengwa kwa udhamini wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) chini ya mpango wa TCRA wa fungu la TEHAMA (ICT-pack) kikiwa na lengo la kutoa huduma za Tehama kwa walimu, wanafunzi na jamii ya kisiwa kidogo cha Tumbatu.
“Matarajio yetu kama serikali tunakwenda kutekeleza dhamira yetu ya dhati, ya kuhakikisha tunatekeleza dira zetu za maendeleo kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na serikali ya Mapinduzi Zanzibar katika kuhakikisha kunakuwa na matumizi bora na matumizi mapana Tehama,” alisema Hamil.
Alisema wizara hiyo itakachofanya ni kuhakikisha inaweka mikakati ya kuhakikisha shule nyingi zaidi na jamii ambazo hazijafikiwa na Tehama zinapata huduma hiyo muhimu katika ukuzaji wa uchumi wa kisasa.
“Niwahakikishie baadhi ya wadau naweza kuwasiliana nao ili kuhakikisha tunakuza Tehama kwa manufaa ya jamii zetu,” alisema
Kwa upande wake, Mkuu wa TCRA Ofisi ya Zanzibar, Esuvatie Masinga akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa mamlaka hiyo wakati wa kukabidhi vifaa vya kituo hicho vilivyowekwa kwenye darasa maalum la kompyuta lililounganishwa na mtandao wa Intaneti alisema, lengo ni kuwafikia wananchi wengi zaidi.
“TCRA Ofisi ya Zanzibar katika kutekeleza mpango huu wa kutoa kwa jamii vifaa vya Tehama, tumeamua kwa awamu hii kujikita kwenye visiwa ndani ya visiwa kwa upande wa hapa Unguja.”
“…tuna vituo viwili tumevifungua; hiki ni kituo cha sita na tuna mpango kwamba mwaka ujao wa fedha tutaomba fedha ili twende kisiwa cha Kojani na maeneo mengine ya Zanzibar lengo likiwa kufikisha huduma za mawasiliano na Tehama kwa jamii kubwa zaidi,” alisema Esuvatie.
Naye, Mkuu wa shule hiyo, Jala Pandu Khamis alisema, kituo hicho si tu kitasaidia ujifunzishaji miongoni mwa wanafunzi lakini pia kitawezesha upatikanaji wa huduma za Tehama miongoni mwa wanafunzi wa shule mbili za sekondari zilizopo kwenye kisiwa hicho.
“Nipende kuwashukuru kwa hisani yenu na kukuahidini kwamba kituo hiki hakitakuwa mali ya shule ya sekondari Tumbatu pekee bali hata wenzetu wengine wa shule ya sekondari Jongowe na wananchi wengine wa kisiwa hiki watanufaika na uwepo wa kituo hiki,” alisema Khamis
Leave a comment