KLABU ya soka ya Simba imefanikiwa kutinga fainali ya michuano ya kombe la Mapinduzi inayofanyika visiwani Zanzibar kufuatia kuondoka na ushindi wa mabao 2-0, kwenye mchezo wa nusu fainali dhidi ya Namungo FC. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)
Mchezo huo wa nusu fainali ya pili ya michuano hiyo ulipigwa hii leo tarehe 10 Januari 2022, kwenye Uwanja wa Amani, majira ya Saa 2:15.
Katika mchezo huo ambao Simba walifanikiwa kutawala katika dakika 90 za mchezo, walifanikiwa kupata mabao yao kupitia kwa Meddie Kagere kwenye dakika ya 15 na bao hilo kudumu hadi mapumziko.
Kipindi cha pili kiliporejea Simba waliendelea kutengeneza mashambulizi nakufanikiwa kuandika bao la pili kupitia kwa Pape Ousmane Sakho kwenye dakika 49 za mchezo.
Kwa matokeo hayo Simba itakuwa inatingga hatua hiyo ya fainali kwa miaka miwili mfululizo ambapo kwa msimu huu itamenyana na Azam Fc ambao waliifunga Yanga kwa changamoto ya mikwaju ya penati 9-8.
Mchezo huo wa Fainali utapigwa tarehe 13 Januari, 2022 kwenye Uwanja wa Amani, kuanzia majira ya saa 2:15 usiku.
Leave a comment