SIKU za Mkurugenzi Mkuu wa Bohari Kuu ya Dawa (MSD) zinahesabika. Ndivyo unavyoweza kusema, baada ya Rais Samia Suluhu leo Jumatano tarehe 6 Aprili 2022 kukumbushia utekelezaji wa maagizo yake ya kuifumua taasisi hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Leo ameenda mbali zaidi na kueleza kuwa anatambua sehemu moja ya utekelezaji ni jukumu lake na kwamba ataenda kulitekeleza haraka.
Rais Samia ametoa kauli hiyo katika uzinduzi wa mfumo wa usafirishaji wa dharura wa wajawazitio na watoto wachanga (M-Mama) ambapo alikuwa akielezea jitihada za Serikali katika ujenzi miundombinu ya afya, kusambaza vifaa tiba na dawa.
“Napenda kuahidi Watanzania kujenga kasi ya mfumo wa huduma bora za afya, kama waziri alivyosema tumeanza na ujenzi wa miundombinu… lakini kazi ya kukunua na kuweka vifaa tiba inaendelea, utafutaji wa dawa yametajwa mabilioni hapa tuliyotoa kwaajili ya dawa lakini bado kuna mapungufu.
“Juzi nilipotoa agizo la wizara ya afya kuangalia mifumo, nilitoa agizo pia la kuangalia MSD haraka sana, najua sehemu moja ni yangu, nakuahidi kwamba nitaifanya haraka,” amesema Rais Samia.
Itakumbukwa kwamba hivi karibuni akipokea Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa mwaka wa fedha 2020/21, Rais Samia alimuagiza Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Hussein Katanga, kuifumua upya kuanzia uongozi wa juu hadi Idara zake.
Hata hivyo kwa mujibu wa Sheria za nchi Rais ndiye mwenye mamlaka ya uteuzi na kutengua nafasi ya Mkurugenzi Mkuu wa taasisi hiyo.
Leave a comment