WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amewasilisha Bajeti ya Ofisi yake na Mfuko wa Bunge kwa mwaka wa fedha 2022/23 zote zikiwa na ongezeko ukilinganisha na bajeti yam waka 2021/22. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Majaliwa amewasilisha bajeti hiyo leo Jumatano, tarehe 6 Aprili 2022, bungeni jijini Dodoma.
Ameliomba Bunge kukubali na kuidhinisha Sh.148.89 bilioni za Ofisi ya Waziri Mkuu ikiwa ni ongezeko la Sh.32.1 bilioni ikilinganishwa na Bajeti ya mwaka 2021/22 ya Sh.116.78 bilioni.
Amesema, kati ya Sh.148.89 bilioni, Sh.101.36 bilioni ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na Sh.47.52 bilioni ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo.
Katika bajeti ya 2021/22, fedha za matumizi ya kawaida ilikuwa Sh.93.3 bilioni na Sh.23.48 bilioni ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo.
Aidha, Majaliwa ameliomba Bunge liidhinishe Sh.132.72 bilioni kwa ajili ya Mfuko wa Bunge ambapo imeongezeka kwa takribani Sh.3 bilioni ikilinganishwa na bajeti ya 2021/22 ya Sh.128.87 bilioni.
Kati ya Bajeti ya 2022/23, Sh.127.32 bilioni ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na Sh.5.4 bilioni ni kwa ajili Matumizi ya Maendeleo. Wakati bajeti ya mwaka 2021/22 fedha za matumizi ya kawaida ilikuwa Sh.121.87 bilioni na Sh.6.99 bilioni kwa ajili ya maendeleo.
Hii ina maaana, Bajeti ya Maendeleo kwa mwaka ujao wa 2022/23 wa Mfuko wa Bunge imepungua kwa takribani Sh.1.5 bilioni.
Leave a comment