SHEIKH Ali Amini, Imamu mashuhuri Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), amepigwa risasi na kuuawa hapo hapo wakati akiswalisha swala ya Magharibi, mjini Beni. Inaripoti mitandao ya kimataifa…(endelea).
Taarifa zinaeleza, mtu mwenye silaha, alimfyatulia risasi Sheikh Ali wakati wa swala ya Magharibi juzi Jumamosi, tarehe 1 Mei 2021, baada ya kufanya tukio hilo, alikimbia.
Mashariki mwa Congo imekumbwa na hali mbaya ya usalama, ikiwemo mashambulizi yanayodaiwa kutekelezwa na kundi la IS.
Makundi mengi yenye silaha yanayoendesha operesheni zao nchini humo, yametokana na mizozo iliyokumba nchi hiyo miaka ya 1990.
Kifo cha Sheikh Ali, kimesababisha mshtuko mkubwa katika mji huo wenye wakazi wapatao 200,000.
Mwanaharakati wa haki za binadamu mjini humo, Stewart Muhindo, amesema tukio hili ni la kwanza kutokea mjini humo.
”Ilitokea wakati wa swala ya Magharibi. Risasi zilifyatuliwa ndani ya msikiti na kumpata Imam. Mtu huyo alitoka eneo la tukio, alikuwa na mwenzake ambaye alikuwa akimsubiri na pikipiki,” Mwanaharakati Muhindo.
Kundi linalohusiana na IS katika eneo hilo liitwalo Kundi la Waasi la Kiislamu (ADF), linahusishwa na mauaji hayo.
ADF iliundwa zaidi ya miaka 20 iliyopita katika nchi jirani ya Uganda, kwa lengo la kupambana na madai ya ubaguzi dhidi ya Waislamu. Lilifurushwa na jeshi la Uganda.
Leave a comment