LAZARO Nyalandu, aliyerejea Chama Cha Mapinduzi (CCM), amemshauri, Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kutoweka masharti magumu ya kwenda kuonana na Rais Samia Suluhu Hassan. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Ni baada ya Rais Samia, kukubali barua ya Mbowe ya kuomba kukutana naye ili kuzungumza masuala mbalimbali hususan ya kukuza demokrasia na utawala bora.
Nyalandu aliyerejea CCM, tarehe 30 Aprili 2021, akitoka Chadema alikokuwa mwenyekiti wa chama hicho, Kanda ya Kati, ametoa ushauri huo, leo Jumatatu 3 Mei 2021.
Alikuwa akihojiwa katika kipindi cha Clouds360 cha Clouds Televisheni.

“Nawasihi Chadema, waache kuweka masharti magumu ya kuonana na Rais, mkuu wa nchi akitaka kukuona usiweke masharti,” amesema Nyalandu, aliyewahi kuwa waziri wa maliasili na utalii, katika utawala wa Jakaya Kikwete.
Katika kusisitiza hilo, Nyalandu amesema “wekeni masharti pembeni, nendeni mkamsikilize, nchi hii ina Rais mmoja.”
Akijibu swali aliloulizwa, iwapo akikutana na Mbowe kwa sasa, atamwambia nini, Nyalandu amesema “nitamchukua tukanywe kahana.”
Amesema, wakiwa kwenye kahaha nitamwambia “wasimwekee masharti, waende wakakutane na Rais ili wamsikilize.”
Tarehe 22 Aprili 2021, Rais Samia akilihutubia Bunge la Tanzania, alisema anakusudia kukutana na viongozi wa vyama vya siasa ili kujadiliana nao masuala mbalimbali yenye maslahi mapana na nchi.
Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika, katika ukurasa wake wa kijamii wa Twitter, alisema baada ya Rais Samia kukubali ombi la Mbowe, wanasubiri kupangiwa siku ya kwenda kuonana naye.
Leave a comment