KUFUATIA ombi la Wakala wa Majengo Tanzania kutaka Serikali kuiwezesha kupata fedha za kuendeleza maeneo ya kota yaliyotwaliwa na Serikali Kuu kutoka Tamisemi, Rais Samia Suluhu Hassan ameitaka kushirikiana na sekta binafsi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
TBA kupitia Mtendaji Mkuu wake, David Kondoro, ameiomba Serikali kufanya hivyo ili kutekeleza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi akinukuu ibara ya 55 (h)(ii) inayoelekeza Serikali kupitia TBA kujenga makazi ya watu wengi kwenye maeneo yaliyotwaliwa na Serikali Kuu kutoka Tamisemi.
Akijibu maombi hayo leo Jumatano tarehe 23 Machi 2022, katika uzinduzi wa nyumba za Magomeni Kota , Rais Samia aliitaka TBA pamoja na taasisi zingine za Serikali zinazioshughulikia ujenzi wa makazi ya watu kushirikiana na sekta binafsi za nje au ndani.
Amesema kwa kufanya hivyo zitaweza kuendeleza makazi bora kwa haraka kuliko kusubiri Serikali kukusanya fedha ambazo haziwezi kukidhi uhitaji wa haraka wa makazi hayo.
“Niliwahi kusema kule nyuma, popote pale ambapo sekta binafsi wanaweza kuweka fedha Serikali tutajitahidi kutoa nafasi kwa sekta binafsi na hivi ninavyozungumza sekta binafsi wapo tayari kushirikiana nanyi TBA na kujenga maeneo yote ambayo mtasema haya yanahitaji kujengwa,” amesema Rais Samia.
Amezitaka pia Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) na Watumishi House kuwakaribisha sekta binafsi ili kuongeza kasi ya maendeleo ya makazi.
“Kaeni na sekta binafsi ya ndani au ya nje mkubaliane kuendelea maeneo yote ambayo yako wazi na ambayo yanapaswa kuendelezwa, kwasababu tukisema tunataka kuendeleza kwa Serikali itatuchukua muda mrefu kutafuta fedha za walipa kodi zichangwe, mjenge itachukua muda,” amesema Rais Samia.
Leave a comment